0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Feb 12, 2010

MUUAJI SHOGA ALIYEPUKUTISHA WENZIE.

Gianni Versace

Wakati mbunifu maarufu wa mavazi duniani, Gianni Versace alipouawa kwa kupigwa risasi nje ya mlango wa nyumba yake katika jiji la Miami, nchini Marekani, polisi walituhumu moja kwa moja kwamba ni mauaji ya kupangwa.

Lakini hata hivyo baadaye waliachana na nadharia hiyo na kumgeukia mtuhumiwa mmoja, aliyekuwa akiendesha mauaji ya watu mbalimbali katika majimbo kadhaa nchini Marekani.

Ilikuwa ni asubuhi ya Julai 15, 1997, kama kawaida yake, Gianni Versace alitoka kwenye jumba lake la kifahari, lililopo ufukweni na kuelekea kwenye mghahawa uliopo karibu na hapo kwake. Alipofika pale alinunua magazeti na baadae alikunywa kahawa na kisha kurejea nyumbani kwake.

Ilikuwa ni kama saa 3 asubuhi wakati anapandisha ngazi za nyumbani kwake, ndipo muuaji alipomtokea kwa nyuma akiwa na bastola na kumpiga risasi mbili kichwani na kisha kutoweka, bila hata kuonekana. Versace alikimbizwa hospitalini na jirani zake waliomwona akigaagaa pale chini huku damu zikimtoka, lakini madaktari wa hospitali ya Jackson Memorial hawakufanikiwa kuokoa maisha yake. Alikufa.

Kwa wale wasiomjua Gianni Versace, labda niwaelezee kwa kifupi kwamba yeye ni nani? Kama wewe ni mfuatiliaji wa wabunifu wa mavazi, naamini kabisa ushawahi kukutana na pafyum, mikoba ya kike, suruali za dangrizi, maarufu kama Jeans, pochi na hata nguo za ndani zenye lebo ya Gianni Versace.

Huyu alikuwa ni miongoni mwa wabunifu wa mavazi, waliojizolea umaarufu kwa kubuni mitindo ya mavazi ya watu maarufu, kama hayati Princess Diana, Elton John, pamoja na waigizaji wa filamu huko Hollywood.

Akiwa na umri wa miaka 50, Gianni Versace alikuwa katika kilele cha mafanikio na utajiri wake alikadiriwa kufikia zaidi ya dola million 500 {kama shilingi za Tanzania bilioni 600}, pamoja na majumba yake ya kifahari yaliopo, Miami, mahali alipouawa, New York na Milani, nchini Italia alikozaliwa.

Kifo chake kiliwashtua watu wengi maarufu hasa Princess Diana, Elton John na Gloria Estafan ambao inasemekana waliwahi kumshauri Gianni Versace ajiwekee walinzi kwa ajili ya usalama wake, lakini alikataa kwa madai kwamba, hataki kuingiliwa uhuru wake.

Ukweli ni kwamba Gianni Versace alikuwa ni shoga na hata katika mojawapo ya mahojiano yake na jarida la Vague alikiri kwamba yeye ni shoga na kumtambulisha mtu mmoja aliyejulikana kwa jina la Antonio D’Amato kama mpenzi wake wa muda mrefu, mtu ambae gazeti mmoja la udaku nchini Marekani liliwahi kumtuhumu kwamba alikuwa pia ni bwanaake dada yake Gianni Versace, aitwaye Donatela Versace, kabla hajaanza uhusiano na Gianni Versace.

Kama nilivyoeleza hapo awali kwamba, mauaji ya Gianni Versace yalihusiswa na mauaji ya kupangwa, msemaji wa polisi wa Miami, Richard Barreto alidai kwamba ushahidi wote wa awali uliokusanywa kutoka kwenye eneo la tukio ulionyesha kwamba mauaji yale yalipangwa kwa umakini wa hali ya juu. ilionekana wazi katika upelelezi wa awali kwamba, Versace aliuawa na mtaalamu wa mauwaji ya kupangwa anayejua ni nini anachokifanya.

Na polisi waliamini hivyo kwa sababu, kuna wakati Versace alituhumiwa kuhusika na genge la maharamia, wanaoendesha uharamia katika biashara ya ubunifu wa mavazi, na hata kuna wakati waliwahusisha wazazi wa Versace ambao ni matajiri wanaomiliki viwanda vya nguo nchini Italia kwamba wanashirikiana na mtoto wao kuvusha dawa za kulevya.

Kwa ujumla biashara ya ubunifu wa mavazi ulihusishwa na biashara ya dawa za kulevya, hivyo haikuwa ajabu kwa Versace kutuhumiwa kuhusika na magenge hayo.

Versace mwenyewe aliwahi kuzikanusha tuhuma hizo. ‘watu wanasema mimi ni ‘mafioso’ hii inaniumiza sana, na inaiumiza hata familia yangu pia.’ Alisema. Lakini, Polisi hawakusita kulitazama hilo kwa sababu wakati wa mauaji yake alikuwa anachunguzwa na polisi kutokana na tuhuma za kukwepa kodi.

Wapelelezi wa Miami walijua kwamba kama mauaji yale yalikuwa ni ya kupangwa, basi kulikuwa na kazi kubwa ya kumkamata muuwaji, kwani kwa mujibu wa takwimu za Florida, jimbo ambalo ndipo mji Miami ulipo, kuna kesi zipatazo 300 za mauaji ya kupangwa, na karibu nusu yake watuhumiwa hawajakamatwa, na hii inatokana na kwamba wauwaji wanatokea katika majimbo ya mbali ambapo huingia jimboni Florida, kuuwa na kisha kutoweka kabisa bila kuacha ushahidi wa kuwatia mbaroni.

Majira ya mchana siku yalipotokea mauaji ya Versace, polisi waliokota nguo ambazo kwa mujibu wa watu wanaoishi jirani na Versace, walikiri kumwona mtu aliye kuwa amevaa nguo zinazofanana na zile zilizookotwa, akisalimiana na Versace, mtu ambaye polisi walianza kumhisi kuwa ndiye muuwaji.

Lakini nadharia hiyo iliwashangaza polisi kwamba iweje muuwaji makini aache nguo zake kwenye eneo la tukio? Je atakuwa ni mzembe kiasi gani?

Hapo tena wakaanza kujenga wasiwasi mwingine kwamba, huenda Versace ameuwawa na mmojawapo wa wapenzi wake.

Hadi kufikia usiku wa siku mauaji yalipotokea, FBI walishajenga hoja nyingine kwamba huenda Versace akawa ameuawa na na muuaji shoga aitwae Andrew Cunanan, anayeendesha mauaji nchini Marekani akiwa amewalenga mashoga wenzie na mpaka kufikia siku Versace anauawa alikuwa ameshauwa watu wanne katika maeneo ya Minnesota, Illinois na New Jersey.

Alikuwa amewekwa kwenye orodha ya watu muhimu kumi wanaotafutwa nchini Marekani na FBI. Cunanan aliyetambuliwa kama kijana mwenye umri wa miaka 27 wakati huo, akiwa na urefu wa futi 5 na inchi 10, alihusishwa na mauaji ya Versace moja kwa moja.

Na hii ilitokana na kwamba, huenda alikuwa na chuki kwa mashoga wenzie baada ya kupimwa na kuonekana ni muathirika wa Ukimwi, kwani watu wote aliotuhumiwa kuwauwa akiwemo Versace walikuwa ni mashoga.

Kutokana na kuwa mtu muhimu anayetafutwa, FBI ilitangaza dau la dola 40,000 kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa zitakazopelekea kukamatwa kwake. FBI walitawanya picha zake tofauti tofauti zikiwemo zile ambazo alivaa mavazi ya kike kwenye majimbo yote ya Marekani.

Siku mbili baadae tangu mauaji ya Versace, Cunanan alionekana kushambulia tena Miami .

Polisi walipata taarifa za kuonekana mtu anayefanana naye akikimbia kutoka kwenye jumba la kifahari lililokuwa umbali wa kama kilomita 16 kutoka nyumbani kwa Versace.

Polisi walivamia katika jumba hilo na kukuta mwili wa mtu aliyekuja kujulikana kama Silvio Alfonso aliyekuwa na umri wa miaka 44, daktari mhamiaji kutoka nchini Cuba, Mwili wake ulikutwa ukiwa nusu uchi sakafuni………..

ITAENDELEA ………………

No comments:
Andika Maoni Maoni

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi