0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Jul 26, 2013

WANAUME HAWAOI SURA TENA BALI UELEWA....!

Wanaume hawaoi sura tena bali uelewa…!

Siku za nyuma, wanaume walijali zaidi uzuri wa sura na mwili wakati walipokuwa wanatafuta mke. Lakini utafiti uliofanywa duniani kote unaonesha kwamba, wanaume hivi sasa wamebadili mitazamo na kuanza kuangalia vitu vilivyo zaidi ya uzuri wa sura na mwili.


Watafiti kutoka Chuo Kikuu cha Grand Valley kilichopo jimboni Michigan nchini Marekani walioendesha sehemu kubwa ya utafiti huo wamesema, wanaume hivi sasa wameanza kujali uwezo wa wanawake katika kufikiri na kujua namna ya kujenga maisha kuliko kujali sura zao na maumbile.



Tafiti nyingi, ukiwemo huo wa karibuni wa Chuo cha Grand Valley, zinaonesha kwamba, kwenye miaka hadi 1980, wanaume walikuwa wakioa wake ambao wanaume hao wanawazidi kielimu na hata kimapato. Lakini kufikia mwaka 2002, wanaume wengi walikuwa wameoa wanawake ambao wanawazidi kielimu, kimapato au kukaribiana.


WANAUME WENYE WAKE WAZURI, HUWA NA 'NYUMBA NDOGO' ZISIZOTAZAMIKA KWA SURA AU UMBO.....!

Wanaume wenye wake wazuri, huwa na ‘nyumba ndogo’ zisizotazamika kwa sura au umbo…..!

Kwa mujibu wa utafiti wangu nilioufanyia kwenye eneo langu la kazi na kwa majirani zangu nimebaini kwamba, kati ya wafanyakazi watano niliofuatilia nyendo zao, ni wawili ambao walikuwa na ‘nyumba ndogo’ nzuri na zenye mvuto kuliko wake zao. Watatu walikuwa na ‘nyumba ndogo’ ambazo zinaweza kumpelekea mtu kujiuliza inakuwaje mwanaume huyo kuwa na ‘nyumba ndogo’ hiyo ambayo hata kwa mbali sana haiwezi kulingana na mkewe. Kwa jirani zangu wanne hali haikuwa nzuri, kwani hapa watatu walikuwa na ‘nyumba ndogo’ zilizo kinyume na wake zao kwa sura na umbo.

Watu saba niliowahoji kuhusu jambo hili, watatu walisema kwamba, wana ushahidi kuhusu wanaume wanaowafahamu wenye ‘nyumba ndogo’ zisizotazamika ukilinganisha na wake zao. Wengine wanne walitoa ushahidi wa wanaume wanaowafahamu ambao wana ‘nyumba ndogo’ nzuri sana ukilinganisha na wake zao.


Ni kitu gani kinatokea?


Ni kwamba, kuna ukweli kuwa wanaume wanaweza kuacha wake zao wazuri sana nyumbani na kufuata wanawake wabaya wasiotazamika kwa sura na umbo huko nje. Lakini pia wanaweza kuacha wake zao wabaya kwa sura ndani na kwenda kufuata wanawake wazuri kwa sura na umbo huko nje.

Hii ina maana gani?

Hii ina maana kwamba kuna mkanganyiko kwenye jambo hili. Lakini kwa bahati nzuri mkanganyiko huu kamwe siyo mkubwa na unaoweza kuumiza kichwa cha mtu. 


Binadamu ana kitu kiinachoitwa ukinaifu. Ukinaifu ni hali ya mtu kuchoka kukiona kitu kilekile mara zote. Kwa mfano, mtu anaponunua nguo mpya leo huipenda sana. Lakini baada ya muda fulani, ikiwa bado haijachakaa hujikuta kiwango cha kuipenda kikishuka.

Lakini ni vizuri nikarudi nyuma na kusema kwamba, kwenye suala la mapenzi. Ukinaifu huwapata wanaume kuliko wanawake. Inawezekana sababu ni za kimaumbile na hivyo ni vigumu kusema ni kwa nini inakuwa hivyo.


Kwa sababu ni suala la kimaumbile inakuwa kama lazima kwa mwanaume kupata ukinaifu. Anapopata ukinaifu siyo lazima atoke nje, yaani dawa yake au ufumbuzi siyo kutoka nje ya ndoa, ingawa wanaume wengi hufanya hivyo. Wanapofanya hivyo siyo kwamba, wanajua kwamba, wamepata ukinaifu, hapana. Wao hudhani tu kwamba, wamempenda mwanamke fulani kwa sababu hizi au zile.
Nadharia moja kuhusu ukinaifu ni kwamba, ili ukinaifu ushibishwe ni lazima mtu apate kitu kilicho kinyume na kile ambacho kimempa ukinaifu huo, au kuwa nacho mbali kwa muda fulani. Kwa mfano, kama mwanaume amepata ukinaifu wa umbile la mkewe ambaye ni kimbaumbau, ni lazima kama ataamua kwenda kutafuta mwanamke wa nje, atatafuta mwanamke tipwatipwa.

Kwa mkabala huo, ndiyo pale tunapokuta mwanaume akimfuata mwanamke wa nje mbaya ukilinganisha na mkewe. Labda anaamua kumfuata mwanamke huyo kwa msukumo wa ukinaifu – amekinaishwa na umbo au sura ya mkewe na hivyo angetaka kuona sura ya aina nyingine, ili afute ukinaifu wake. Kinyume cha sura nzuri ni sura mbaya, kwa hiyo atatafuta mwanamke mwenye sura kinyume na ile ya mkewe.
Kuna ukinaifu wa aina nyingi kwenye maisha ya ndoa. Mwanaume anaweza akakinaishwa na mtindo wa nywele wa aina moja wa mkewe. Kama mwanaume huyu hatakuwa mwangalifu, atajikuta akitafuta ‘nyumba ndogo’ yenye mtindo tofauti na mkewe. Inawezekana mkewe anatumia mtindo wa ‘twende kilioni’ kila akisuka nywele zake. Mwanamume anapokwenda kutafuta kilicho kinyume huko nje, anaweza akajikuta amevutiwa na mwanamke mwenye kunyoa na kuchana nywele zake fupi.

Kwa hiyo, inawezekana kabisa mwanaume akatoka nje ya ndoa yake kutafuta kinyume ambacho siyo sura wala umbile. Inawezekana akatoka kwa sababu amekinaishwa na ukimya wa mkewe, hivyo anatafuta kelele. Huyu anaweza kujikuta akiwa na mwanamke wa nje muongeaji na chakaramu sana, ambaye kisura na kiumbile anaweza kuwa sawa na mkewe.

WANAWAKE: WANAUME WANAPOWABISHIENI MSIWASHANGAE...!

Kwa nini wanaume ni wagumu sana kufanya mambo ambayo wake zao wanawaomba au kuwataka kufanya? Jibu, ni kwa sababu ni wanaume na wameona baba zao wakifanya hivyo na wakaiga. Lakini jibu linaweza kuwa lingine, kutegemea na ufahamu wa mtu na hata mazingira. Lakini ukweli unabaki kwamba wanaume sio wepesi wa kutenda yale ambayo wanatakiwa na wake zao kutenda. 

Taarifa za kiutafiti zinaonesha kwamba, mwanaume ni mgumu kufanya anayotakiwa au kuombwa na mkewe kufanya kwa sababu nyuma ya ubongo wake, kuna kizuizi. Inadaiwa kwamba ubongo wa kina wa mwanaume kuna kitu kinachopingana na chochote ambacho mwanamke anamtaka kufanya.



Siyo suala la kurithi, hapana. Ukweli ni kwamba, kutokana na mwanaume kutokuwa tayari kuongozwa au kumsikiliza mwanamke na kumkubalia, hatimaye imejijenga akilini na kuwa kama vile ni suala la maumbile. Ukweli ni kwamba, miaka mingi ya kutoamini kwamba, mwanamke anaweza, imefanya kuwe na kizuizi hicho kwenye akili ya mwanaume.


Utafiti wa hivi karibuni kwa mfano, ambao uliongozwa na Gavan Fitzsimons profesa wa masoko na saikolojia, kwenye chuo kikuu cha Duke, anasema, kinachotokea ni juhudi za mwanaume kutotaka kuingiliwa kwenye mambo yake, bila mwenyewe kujua kwamba, anafanya juhudi hiyo. Jambo hili kisaikolojia linafahamika kama reactance, ambapo mtu hufanya kinyume kabisa na anavyotakiwa kufanya. Ni juhudi za mtu kupinga kupewa amri au kuingiliwa katika uhuru wake. 

Wataalamu wanasema kwamba, wanaume hujikuta tu wamepinga jambo la mke bila kujua hata sababu. Ndio maana wanaume wengi huharibikiwa kwa kukataa kufanya yaliyopendekezwa na wake zao na baadae hujiuliza ni kwa nini walikataa. Kwa hiyo wanaume wanapaswa sasa kujua kwamba, wanapombwa jambo na wake zao au kutakiwa kulifanya, wako kwenye hatari ya kulikataa. Kwa hali hiyo, wanapaswa kuwa waangalifu.

Jul 10, 2013

MWANAMKE: JE UNATAFUTA MCHUMBA? FUATA KANUNI HII, HAKIKA UTAMPATA MCHUMBA MWENYE TABIA UZITAKAZO


Mwanamke: Je, unatafuta mchumba? Fuata kanuni hii hakika utapata mchumba mwenye tabia uzitakazo...

Kuna kitu kinaitwa nguvu ya mvuto, lakini pia huenda mmeshawahi kusikia au kusoma kitabu kinachoitwa “The Secret.” Ni kitabu kizuri sana kinachoeleza kwa kirefu na kwa lugha nyepesi inayoeleweka jinsi nguvu hii ya mvuto inavyofanya kazi. Katika kitabu cha The Secret mwandishi Rhonda Byrne anasema kwamba mawazo yetu ni kama sumaku. Kwa kawaida sisi wanadamu tumezungukwa na nguvu ambazo hatuzioni lakini zipo kwa hiyo Kwa jinsi tunavyofikiri hayo mawazo yanakuwa na nguvu ambazo zinavuta kila kitu tunachowaza, kiwe kizuri au kibaya, ni lazima kitarudi kilipotoka, ambapo sipengine bali kwako wewe mwenyewe.

Rhonda anazidi kubainisha utendaji wa mawazo yetu kwa kutoa mfano wa ufanyaji kazi wa Luninga (TV). Kama wote tunavyofahamu kuwa ili kituo cha kurusha matangazo ya Luninga kifanye kazi kunakuwa na minara inayosafirisha mawimbi na kuyageuza katika mfumo wa picha na hivyo kutuwezesha kuona matangazo ya luninga tukiwa majumbani kwetu. Wengi wetu hatufahamu mitambo hiyo inafanya kazi namna gani, lakini tunafahamu kwamba kila chaneli ina mawimbi yake ambapo kila tukichagua chaneli fulani tunapata picha katika luninga zetu. Tunachagua mawimbi kwa kubadilisha chaneli na ndipo tunapopata picha za matangazo kutoka katika chaneli hiyo. Kama tunataka kuona picha na matangazo tofauti katika luninga zetu tunabadilisha chaneli kwa kutafuta mawimbi ya chaneli nyingine.



Sisi kama wanaadamu tuko sawa na mnara wa kurusha matangazo ya luninga na tuna nguvu kuliko minara ya kurusha matangazo iliyowahi kuwepo hapa duniani. Mawimbi yetu ndiyo yanayoratibu maisha yetu na ndiyo yanayoifanya dunia iwe kama livyo leo, kwani tunatengeneza mawimbi kutokana na namna tunavyowaza. Ile picha tunayopata au tunayoiona kupitia mawazo yetu, sio sawa na ile tunayoiona katika luninga zetu sebuleni kwetu, bali ni picha ya maisha yetu! Mawazo yetu yanatengeneza mawimbi na yanavuta kila tunachokiwaza na kuwa ndio maisha yetu halisi.

Iwapo tunataka kubadili chochote katika maisha yetu, basi inatulazimu tubadili chaneli na mawimbi kwa kubadili namna yetu ya kufikiri. Mwandishi huyo anaendelea kusema, kinachosabisha watu wengi wasipate kile wanachokitaka maishani ni kwa sababu wanafikiria zaidi kuhusu kile wasichokitaka badala ya kile wanachokitaka. Hebu tujaribu kuchunguza mawazo yetu na kauli zetu, tutagundua siri kubwa. Kwani nguvu ya mawazo ipo na inafanya kazi. Ugonjwa mkubwa sana unaowakabili wanadamu hapa duniani karne kwa karne ni ugonjwa wa “sitaki” au “sipendi,” anabainisha mama huyo. “Watu wameendelea kuacha ugonjwa huu uendelee kutawala katika mawazo yao, vitendo vyao na kauli zao, wakiendelea kuzingatia yale wasiyoyataka au wasiyoyapenda.” Anamalizia kusema mwandishi huyo.


Ugonjwa huo ndio unaowatesa baadhi ya wanawake wanaotafuta wapenzi. Mfano halisi ni kauli kama, “mimi sipendi wanaume wafupi,” au “mimi sipendi kuolewa na mwanaume mnyanyasaji….” na kauli nyingine zinazofanana na hizo. Ukweli ni kwamba kitakacho watokea wanawake wenye kutoa kauli kama hizo ni kuishia kuolewa na wanaume wa aina hiyo….. kinachofanyiwa kazi na mawazo yetu ya kina (Unconscious Mind) ni kile tunachokitamka, iwe ndicho tunachokitaka au tusichokitaka, mawazo yetu ya kina hayajui neno sipendi au sitaki, hukuletea kile ulichokitamka na kukijaza katika akili yako. 


Kuna wanawake wengi ambao wameolewa au wamewahi kujenga mahusiano na wanaume ambao waliwahi kutamka hadharani kwamba kamwe hawatoweza kujenga mahusiano nao au kuolewa nao. Hayo ni matokeo ya kauli zao ambazo walizitamka bila kujua madhara yake. Kwa hiyo basi kwa kutumia kanuni hiyo ya mvuto kama alivyosema mwandishi Rhonda Byrne mnatakiwa kuanza kuratibu mawazo yenu na kauli zenu kwa kutamka aina ya wanaume ambao mngependa kujenga mahusiano nao au kuolewa nao na haiishii hapo ni vyema mkajiweka katika mazingira ambayo yatawavuta kuelekea mahali ambapo mtakutana na aina ya wapenzi muwatakao. Huwezi tu kukaa nyumbani kwako au kutembelea eneo moja hilo hilo kila siku halafu utarajie kukutana na aina ya mpenzi umtakaye itakuwa ngumu, labda uwe na bahati sana.

MWANAMKE: KABLA HAJATOA TAMKO LA KUFUNGA NDOA USIMWAMBIE HAYA...


Mwanamke: Kabla hajatoa tamko la kufunga ndoa usimwambie haya…!


Katika maisha wote tuna siri zilizotuzunguka na mambo mbalimbali ya kifamilia pengine yanayotia kinyaa ambayo huwa tunatamani yasijulikane kwa wengine au labda yafutike kabisa. Lakini inategemea unayachukuliaje mambo hayo au yanaathiri vipi mitazamo yako kuhusu wewe. Ukweli ni kwamba hatuwezi kuyabadili labda tunachoweza kufanya ni kubadili mitazamo ya wengine kuhusu yale yaliyotuzunguka…………

Familia yenu ni ya vurugu tupu:
Baba yako ni mlevi kupindukia au baba yako na mama yako wote ni walevi kupindukia. Kaka zako ni mateja au dada zako wote wamezalia nyumbani au waliwahi kuolewa na kuachika, na sasa wako nyumbani tu wakichapa umalaya na pengine wanaendelea kuzalia nyumbani. Haya ni mambo ambayo hupaswi kuyazungumzia kwa mpenzi ambaye hajatoa tamko la kutaka mfunge ndoa. Kwani itamfanya mpenzi mpya atengeneze tafsiri tofauti kuhusu wewe. 

Uhusiano wako wa mwisho na mwenzi wako ulivunjika kwa vurugu:
Inawezekana mpenzi wako wa kwanza mliachana kwa vurugu kubwa, kwa mfano ulifikia hatua ya kufanya jaribio la kunywa sumu kutokana na kugombana kwenu kabla ya kuachana kwenu. Haya ni mambo ambayo hupaswi kuyasema kwa mpenzi wako mpya, kwani utampa maswali mengi sana ya kujiuliza juu yako.

Idadi ya wapenzi uliowahi kuwa nao:

Kuwa na idadi ndogo au kubwa ya wanaume uliowahi kuwa na uhusiano nao haimaanishi kwamba wewe ni mzuri katika mapenzi, sana sana unajidhalilisha tu. 


Maisha yako ya ujanani ya kujirusha:

Maisha yako ya ujanani au ulipokuwa shule ukijirusha kwenye kumbi za starehe ni ya kwako na si vyema uyapigie upatu kwa mpenzi mpya ili akujue kwamba na wewe hauko nyuma katika mambo ya starehe.


Ushawahi kuishi maisha ya kutangatanga:

Ni kumbukumbu yenye kuumiza hisia pale ukumbukapo maisha yako ya utotoni kama yalikuwa magumu na machungu. Kulelewa na wazazi wasiojali na watesaji, kuishi kwa kutangatanga kutoka nyumba moja hadi nyingine kutafuta hifadhi kutokana na kunyanyaswa. Kubakwa au kuishi maisha ya vurugu katika familia. Haya ni matukio ambayo yameshapita na hayatakiwi yatawale fikra zako tena. Umeshakua mtu mzima na maisha yanasonga mbele. Kuanza kumsimulia mpenzi mpya kuhusu aina ya maisha uliyokulia kama yalikuwa ni ya taabu kama nilivyoeleza hapo juu kutamfanya akuone kama wewe utakuwa unatonesheka kihisia haraka kutokana na kujeruhiwa kihisia utotoni. Mpenzi anaweza kukukwepa na hatimaye kukukimbia.

Jul 8, 2013

HII NDIYO SABABU YA WANAWAKE WENGI KUIBUA MABOMU...!

Hii ndiyo sababu ya wanawake wengi kuibua mabomu…!

Mnamo mwaka 1973 Dk. Paul MacLean, mtafiti toka taasisi ijulikanayo kama National Instute of Mental Health, alibaini kwamba, ubongo una sehemu tatu zinazoendana na nyakati tatu za mabadiliko ya kimaumbile.

Sehemu ya kwanza inaitwa reptilian. Hii inahusiana na kukutana kimwili kati mwanamke na mwanaume na tabia ya ukatili, hisia za hasira na hofu. Sehemu ya pili ni limbic brain. Hii inahusika na mapenzi, huzuni na wivu. 


Hata matumaini asili yake ni katika sehemu hii. Sehemu hii ndiyo inayodhibiti mapigo ya moyo na joto. Yote haya huathiriwa na kuwepo mahali hapo na mtu tunayempenda. Hamu ya mapenzi huenda moja kwa moja katika sehemu hii. Ni sehemu ambayo ina pupa na inaenda kasi kama umeme.


Ni enao ambalo halitaki kabisa kujishughulisha na mambo ya kutumia akili au tathmini. Sehemu ya tatu ya ubongo inaitwa neo-cortex, ambayo huruhusu matumizi ya mantiki, kutafakari kwa kina, lugha, kufanya mipango, kufikiri na maamuzi ya kina baada ya kufikiri kwa kina.


Katika kitabu chake cha The Emotional Brain, Joseph LeDoux anasema kwamba, sehemu zile mbili za kwanza za ubongo zinathibiti sana ile sehemu ya tatu. Na wala hii sehemu ya tatu haina udhibiti kwa zile sehemu mbili. Na ndiyo maana katika maisha ya kawaida, ‘hisia hudhibiti fikra.’ 


Ingawa fikra zinaweza kuamsha hisia kirahisi, lakini fikra zinapata tabu sana kuziondoa hisia zikishaingia. Hii ina maana sehemu ya pili ambayo ndiyo inayoziamrisha hisia, inaweza kuiburuza sehemu ya tatu kila inapotaka. Limbic ya mwanamke itamwambia, “umempata mwanaume barabara.” Sawa, lakini mwanaume mwenyewe ni mlevi..! 

Limbic itasema, “Nitaishi naye hivyohivyo. Ana sura nzuri mno, ninajisikia vizuri sana ninapokuwa naye….”

Sasa nafikiri unaweza kuona kwamba, hata kama mwanamke anaweza kusema kwamba anamtaka mwanaume mwenye haiba nzuri na mtu mwema si lazima kwamba, ndiye atakayevutiwa naye. Mfano mzuri wa jambo hili ni chakula.


Je huwa tunakula chakula kufuatana na ubora wake kiafya? Hapana…! Wengi wetu tunakula kutokana na utamu na ladha ya chakula! Dona ni bora kuliko ugali wa mahindi yaliyokobolewa kiafya. Lakini asilimia 90 ya Watanzania wanapenda ugali wa mahindi yaliyokobolewa maarufu kama Sembe. 


Hali hii ndiyo inayompata mwanamke anapofanya uchaguzi na kujikuta akimchagua mwanaume anayemfanya kujisikia raha, lakini ambaye si mtu mzuri kwake.


Suluhisho la jambo hili ni nini….?


Wanawake wanaweza kufanya urafiki na wanaume hao wazuri wa sura na wenye sifa ya uburuzaji na valuvalu kwa idadi wanayotaka kama kwa kufanya hivyo watajisikia raha maishani mwao; ili mradi tu urafiki huo usilete maumivu na huzuni ambayo yako juu kuliko furaha yenyewe. 


Kama huzuni ni kubwa kuliko furaha katika mapenzi na mwanaume aliye naye, basi mwanamke hana budi kuachana na limbic brain na kuchagua mwanaume anayemfaa kwa kutumia mantiki.

KWA NINI WANAUME WENGI SIKU HIZI HAWAPENDI KUOA...?


Kumekuwa na maswali yasiyo na majibu miongoni mwa jamii kwamba imekuaje vijana wa kiume wamekuwa ni waongo sana hasa linapokuja swala la kuoa? Kwa kadiri siku zinavyozidi kwenda ndivyo ambavyo idadi ya wanaume wanaoogopa kuoa inazidi kuongezeka. Utakuta wapenzi wanaambiana kwamba wanapendana na kuahidiana kuwa wataoana, lakini kitakachotokea baada ya hapo ni mwanaume kuanza kupiga chenga kwa visingizio lukuki.

Kwa nini hali hiyo hutokea?

Ukweli ni kwamba hakuna jibu la moja kwa moja juu ya tatizo hilo, lakini yapo mambo ambayo yanaweza kutupa angalau tafakuri. Nitajaribu kudadavua baadhi ya sababu zinazowafanya wanaume siku hizi kukwepa kuingia katika taasisi ya ndoa:

Ukosefu wa mtu wa kumchukulia kama mfano: Hapa nawazungumzia wale watoto wa kiume waliolelewa malezi ya upande mmoja yaani walilelewa na mama peke yao. Sina maana ya kudharau au kutweza malezi ya mama, la hasha, lakini ni vyema mkafahamu kwamba kuwa na baba asiye na malezi mazuri si sawa na kutokuwa na baba. Na ndio maana nikasema ukosefu wa mtu wa kumchukulia kama mfano. Achilia mbali aina ya malezi atakayoyapata kwa familia yawe mazuri au mabaya lakini lazima kutakuwa na tabia za kiume zitakazoakisi malezi ya mtoto wa kiume katika familia husika. Watoto waliolelewa na mama peke yao kuna kitu huwa wanakosa, kwani wanakuwa hawana mtu wa kumchukulia kama mfano kwa upande wa jinsia ya kiume na hapo ndipo hujikuta wakijifunza wenyewe namna ya kuongea na kutenda kama wanaume kwa sababu katika makuzi yao hawakupata fursa ya kuwa karibu na baba zao. Kwa kuwa siku hizi kuna kundi kubwa la kina mama ambao wamejikuta wakiachiwa mzigo wa malezi ya watoto, baada ya aidha kuachwa na waume zao au kuzalishwa na kutelekezwa (Single mothers), na hapo ndipo tunaposhuhudia mtoto wa kiume anapokua kwa umri na kimo huku akiwa hana mtu wa kumuangalia kama mfano wa mume anavyotakiwa kuwa katika familia zaidi ya kujifunza mambo hayo kupitia katika TV, senema au miziki. Wanaume waliopitia malezi ya aina hii huchelewa sana kuoa kwani huyaangalia maisha ya ndoa kwa namna ya kujaribu na ndipo hapo wengi huishia kuishi kinyumba na wanawake kwa ajili ya kutaka kujifunza namna ya maisha ya ndoa yanavyotakiwa kuwa na ndio sababu huchukua muda mrefu kufanya maamuzi. Na mara nyingi huishia kubadilisha wanawake kutokana na kutokuwa na uhakika wa kile wanachokitafuta.

Mgogoro wa kiuchumi: Kuna kundi kubwa la vijana siku hizi hawana ajira au hawana uhakika na kipato. Ukweli ni kwamba hakuna mwanaume atakayependa kujiingiza kwenye ndoa wakati hana kazi au hana uhakika na kipato chake. Na hiyo ni kutokana na wanawake wengi siku hizi kuonekana kujali zaidi wanaume wenye uhakika na kipato. Hii misemo ya wanawake ya kebehi dhidi ya wanaume wasio na ajira au kipato, kama vile “mwanaume suruale” ina mchango mkubwa sana katika kuwafanya wanaume kukwepa kuoa iwapo hawana ajira au hawana uhakika na kipato chao.


Wanawake wengi kuwa na kiwango cha elimu ya juu: Siku hizi wanawake wengi wameibuka katika kutafuta elimu ya juu kwa juhudi kubwa. Idadi ya wanawake wanaojiunga na vyuo vikuu ni wengi tofauti na ilivyokuwa zamani. Na hiyo ni kutokana na wazazi wengi kubadili mtazamo wao juu ya mtoto wa kike. Zamani mtoto wa kike alichukuliwa kama kitega uchumi. Kwa maeneo ya vijijini na katika familia masikini, watoto wa kike walikuwa wanatazamwa kama, ‘biashara ya kesho’ ambapo watauzwa kwa njia ya mahari. Kwa hiyo thamani yao ilikuwa ni kuolewa, ni ile ya kibidhaa na sio kibinadamu. Lakini tofauti na zamani siku hizi hata kule vijijini kumekuwa na mwamko mkubwa sana wa kumsomesha mtoto wa kike hadi elimu ya juu. Kutokana na mwamko huo wanawake wengi wamejikuta wakiona elimu kama kimbilio pekee la kuepukana na mfumo dume. Mwanamke gani atakubali kunyanyaswa na mwanaume akiwa na elimu yake na labda pia akiwa na kazi yake yenye mshahara na marupurupu ya kutosha, naamini watakuwa ni wachache sana ambao hawajiamini au waliathiriwa na malezi. Kwa upande wa wanaume nao, wamejikuta wakiwaogopa wanawake hawa wenye elimu ya juu kwa hofu ya kuzidiwa kipato na labda kukosa sauti kama mwanaume na hiyo inatokana na ego tu. 

Wanaume huwaona wanawake kama tishio wanapokuwa na mafanikio makubwa kifedha: Inaweza kutokea mwanaume anaweza kuwa na uhusiano na mwanamke ambaye labda tu nisema ni mbangaizaji. Wakati huo anaweza kuahidi kufunga ndoa na mwanamke huyo, lakini iwapo itatokea mwanamke huyo akapata mafanikio kibiashara na kuinuka kifedha. Kama mwanamke asipokuwa makini anaweza kusababisha mwanaume huyo akaingia mitini. Sababu kubwa hapo inaweza kuwa ni hofu ya kuogopa kuongozwa na mwanamke. Kumbuka kwamba mfumo dume bado umetawala vichwani mwa wanaume wengi kutokana na malezi. Mwanaume asiyejiamini ni vigumu sana kwake kuoa mwanamke aliyemzidi kipato. Kwa sababu akifanyiwa jambo dogo tu, inakuwa kama ametoneshwa. Atahisi kutaka kutawaliwa na mwanamke huyo. Jambo ambalo wanawake wanatakiwa kulifahamu ni kwamba kila mwanaume anataka kutambuliwa na kuheshimiwa kama shujaa kabla ya kumfuata msichana. Iwapo utakuwa umesimama iwe ni kifedha au kielimu pale unapotafuta kupata mwenza, inabidi ujishushe sana la sivyo utadoda.


Wanaume wengi siku hizi wana hofu ya majukumu, hasa ya kulea watoto: Kutokana na malezi yao au kile wanachokijua kuhusu watoto, baadhi ya vijana huamini kwamba, kulea watoto ni jambo gumu sana. Lakini wengine wanaamini kwamba, hata mke anapaswa kulelewa kama ilivyo kwa mtoto. Hivyo wanaamua kutafuta kwanza uwezo ambao haupatikani kiurahisi. Kuna wengine, ambao wamefundishwa au kuelekezwa na mila na desturi zao kwamba, kabla hawajaoa, ni lazima wawe na nyumba kwanza, tena kwao. Kwa hiyo, hawa hadi waje wapate uwezo wa fedha wanakuwa wameshachelewa.

Kuna baadhi ya wanaume, maisha bila ya ndoa wanayaona kuwa ndiyo bora kuliko yale ya ndoa: Kuna baadhi ya wanawake hujirahisisha sana kwa wanaume. Siku hizi ni jambo la kawaida sana kukuta mwanaume anaishi na mwanamke bila ndoa, wenyewe wanaita Trial Marriage. Na hapo ndipo unapokuta wanaume hawaoni tena umuhimu wa kuoa. Sasa kama mwanamke anaweza tu kuishi na mwanaume bila ya ndoa na mwanaume huyo akapata huduma zote kutoka kwa mwanamke huyo, unadhani ni kitu gani kitamvuta kufunga ndoa. Jambo lingine ni ile dhana kwamba maana ya ndoa ni tendo la ndoa. Siku hizi wanaume wengi wamejikuta wakiwa hawahitaji tena kuoa kwa sababu tendo hilo linapatikana kiurahisi tofauti na zamani. Siku hizi inawezekana kabisa kumtongoza binti leo na kupata tendo siku hiyo hiyo….. Na hapa siwazungumzii makahaba. Nawazungumzia mabinti zetu ambao wengine ukiwaona ni watu wa kuheshimiwa ukiwaangalia kwa nje lakini kwa ndani hawana lolote, vijana wa siku hizi wenyewe huwaita maharage ya Mbeya.

Kuna sababu nyingi zinazotajwa kusababisha wanaume siku hizi kujivuta sana katika kufanya maamuzi ya kutafuta mwenza. Lakini hizo chache nilizozitaja zina mchango mkubwa.

UHUSIANO UNAPOVUNJIKA, WANAWAKE NDIYO HUUMIA ZAIDI....!


Kwa kuangalia idadi ya watu wanaoathirika kufuatia kuvunjika kwa uhusiano kati ya mwanamke na mwanaume mtu atagundua kwamba wanawake ndiyo ambao hupatwa na athari kubwa zaidi. Kwa mfano ukichukua watu ishirini, wanawake kumi ambao wameachwa na wapenzi wao na wanaume kumi ambao nao wameachwa pia na wapenzi wao, utagundua kwamba, wakati ni wanaume watatu tu kati ya hao kumi ndio watakaosumbuliwa sana na na hali hiyo, kwa wanawake idadi itakuwa ni saba kati ya hao kumi. 


Watu wengi wanaweza kukimbilia kwenye kusema hali hiyo inatokana na utegemezi wa wanawake kwa wanaume. Hii ikiwa na maana kwamba, wanaathirika zaidi kwa sababu, kwa kuachwa ina maana pia kwamba hawataweza tena kupata mahitaji ambayo walikuwa wanapewa na wanaume hao. Dhana kama hii inaweza kuwa na ukweli fulani, lakini hali halisi inakataa. Kuna wanawake ambao wana uwezo mkubwa nap pengine ndiyo wanaowalisha na kuwavisha wanaume, lakini wanapoachwa na wanaume hao huathirika sana. 


Wanawake wa aina hii inadaiwa kwamba huathirika zaidi kuliko wale walio tegemezi. Kuathirika huku kwa ziada huhusishwa kwa kiasi kikubwa na ukweli kwamba wanaume ni watu wa kutoa ili kupalilia penzi, lakini hapa badala ya kutoa wanapewa na bado wanaondoka. Hili huwatanza wanawake wa aina hii. Lakini sababu ambayo huenda wengi wetu tulikuwa hatuijui kuhusiana na suala hili la wanawake kuathirika zaidi baada ya kuvunjika kwa penzi au kuachwa ni ‘ndoto.’ Kimaumbile wanawake huota zaidi ndoto za mchana au hufikiria zaidi kuhusu maisha yao ya kimapenzi yatakavyokuwa ukilinganisha na wanaume. Siyo kufikiria tu, bali hufikiria kwa njia inayoonyesha kuwa maisha hayo yatakuwa kama peponi.



Wanawake, wakiwa bado wasichana (baada ya kuvunja ungo) huanza kufikiria na kupiga picha jinsi busu lao la kwanza litakavyokuwa, mtu ambaye watabusiana awali. Hufikiria pia kuhusu wapenzi wao wa awali watakavyokuwana jinsi itakavyokuwa watakaposhiriki nao tendo kwa mara ya kwanza na huwa wanapiga picha ya jinsi siku yao ya harusi itakavyokuwa na watu watakaowaona. Katika kupiga picha huko huwa wanafikiria namna ambavyo mambo hayo yote yatakavyoenda vizuri bila doa, huwa wanajiona wakiwa wamefanikiwa katika hatua zote na hatimaye kuishi kwa raha mustarehe milele na watakaokuwa wapenzi wao. Kwa upande wa wanaume hakuna ndoto za aina hii na hata kama zipo ni kwa wachache sana, wakati kwa wanawake ni kama sehemu ya makuzi kwao. 


Kwa hali hiyo, ukiacha mazingira wanamokulia wanawake, kwa sehemu kubwa hukua wakiwa na hizo ndoto zao, ambazo kwao siyo ndoto bali ukweli. Wanapokuja kwenye ukweli wa uhusiano hugundua kwamba busu la awali siyo kama walivyotegemea liwe, mpenzi wa awali siyo kama walivyomtegemea awe na wala maisha ya ndoa siyo matamu kama walivyokuwa wameota. Kwa kuwa hawakujiandaa wala kutegemea mazingira magumu ya uhusiano, hawakuwa wakiota kuhusu ugumu wa uhusiano bali wororo, wanapokutana na masuala ya kuvunja moyo kama kuachwa hubabaika sana. Kwa kuwa akilini mwao walikuwa na picha ya mafanikio katka uhusiano, kushindwa kwa uhusiano, huwafanya wajione kwamba, wao ndiyo wakosaji, wameshindwa kulinda uhusiano ambao katika ndoto zao waliamini kwamba ni mzuri na usio na doa 


Ukiangalia kwa makini katika uhusiano, wanawake ndio wanaojitahidi sana kulinda uhusiano usivunjike, wao ndiyo wavumilivu zaidi, ndiyo ambao hujitahidi kuyarudisha mambo yaende sawa pale yanapokwenda kombo hata kama kufanya hivyo kunawagharimu. Yote hii ni juhudi yao ya kutaka kuishi kwa kadiri ndoto zao za kabla zilivyowaonyesha, kwamba uhusiano kati ya mwanamke na mwanaume ni mtamu, mororo na usio na chembe ya doa……

Jul 7, 2013

MWANAMKE: HATA KAMA HUZAI KINAKUUMA NINI...?


Mnaweza kufikia umri huu bila mtoto na ndoa ikaendelea kuwa ya upendo.......


Inaelezwa kwamba wanawake huwa wanavurugikiwa sana kiakili pale wanapogundua kwamba hawana kizazi au hawawezi kupata watoto.


Kuna ukweli kwamba mwanaume kama mwanamke huwa anasikitishwa na kukosa mtoto katika ndoa lakini kwa bahati mbaya tafiti mbalimbali zinaonyesha kwamba mwanamke huathirika zaidi kwa kujaribu kwake kuikataa hali hiyo. Wanawake huchukulia suala la kukosa mtoto au watoto kama ndio mwisho wa maisha yao.



Sio kwamba wanaume hawaumii kwa tukio kama hilo, la hasha huumia sana, lakini kinachotokea ni kwamba wao hulichukulia kwa uzito wa kawaida na hii husaidia kupandisha kiwango cha uwezekano kwao kupata ufumbuzi au suluhu ya tatizo hilo.



Wanawake mara nyingi wamekuwa wakihesabiwa kama ndio chanzo cha matatizo ya ndoa zisizo na watoto na kwa bahati mbaya wanawake wameonekana kwa kiasi kikubwa kuamini lawama hizo. Jambo hili huenda ndilo ambalo linawafanya wanawake kukosa raha kabisa pale wanapokuwa hawana watoto ukilinganisha na wanaume. Wanawake huogopa kwamba kwa kukosekana watoto ndani ya ndoa waume zao wanaweza kuchukua uamuzi wa kuoa wake wengine na kuwaacha wao au wao kuwa wake wakubwa wasio na thamani. 



Hii ni njia ambayo imekuwa ikitumika sana katika mila karibu zote za Kiafrika. Lakini jambo kama hili halipaswi kuogopwa sana na mwanamke kwa sababu mume anayeamua kwenda kuoa mke mwingine kwa sababu mkewe wa awali hakubahatika kupata mtoto, huyo ni mwanaume asiye na upendo. Kwa nini basi mwanamke asione hiyo ni nafuu kwake ya kuachana na mtu ambaye alikuwa akiishi naye bila upendo.



Kwanza siku za nyuma wakati wa ujima mwanamke angeweza kulalamika sana kukosa mtoto, kwani mtoto alikuwa ni rasilimali. Lakini siku hizi mtoto ni sehemu ya ukamilisho wa jukumu la kimaumbile la mtu kulea kama alivyolelewa. Kama mwanamke anajikuta hana mtoto anaweza kwenda kuchukuwa mtoto kwenye nyumba za watoto yatima au kuomba ustawi wa jamii ili apewe mtoto aliyetupwa au kutelekezwa na wazazi. Huyu naye ni mtoto sawa au kumzidi yule wa kumzaa kama atapata malezi mema.



Imefika wakati ambapo inabidi wanawake wajue kwamba kukosa mtoto au watoto siyo mwisho wa dunia na wala haiwapunguzii hata chembe ya utu wao.

ALINIPIGA KIDOGO TU, TENA MARA MBILI KWA MWEZI, KUNA WANAOPIGWA KILA SIKU...!


Tunajua wote kwamba, hutokea wanawake wakateswa sana kwenye uhusiano wao wa kindoa au kimapenzi na bado wakaendelea kukaa tu kwenye uhusiano huo. Inafikia hadi mtu anakufa huku akiona kabisa. Watu wengine huiita hali hii kuwa ni ujinga na wengine huita kulogwa au huelezea hali hii kwa njia ambayo haiwapi haki wanawake hao. Zipo sababu nyingi ambazo zinawafanya wanawake kuendelea kukaa kwenye ndoa ngumu, bila hata kufikiria kuondoka. Sababu nyingine zinaweza kuonekana kama kituko, lakini ndizo zinazowafanya wafie kwenye ndoa.

Kuna ile sababu kwamba, hawajui ukubwa wa kiwango cha mateso. Hii hutokana na kwamba, baada ya kuzoea mateso, mwanamke hufikia kuamini kwamba, hayo siyo mateso, bali ndivyo ndoa inavyotakiwa iwe. Kuna sababu ya kukosa marafiki, ndugu au jamaa wa karibu. Na kwa sababu hana watu wa aina hiyo, inakuwa vigumu kwake kuwa na mahali pa kukimbilia ili aweze kupata nafasi ya kujiandaa kuanza upya maisha. 


Kuna wanaoendelea kukaa kwa sababu dini zao zinawaambia, hawana budi kukaa, kwani wameshakuwa mwili mmoja na waume zao na hivyo hawawezi kuondoka. Wanafikiria iwapo wataamua kutoroka, viongozi wao wa dini watawaona vipi na waumini wenzao watachukuliaje jambo hilo. Kwa hiyo, wanaishi kwenye ndoa hizo kwa sababu ya dini, siyo kwa sababu yao binafsi. Halafu kuna suala la kupenda. Utegemezi wa kihisia huwa unaitwa kupenda. Kwa hiyo mwanamke anasema anampenda fulani kiasi kwamba, hawezi kumwacha, wakati ukweli ni kwamba, anamtegemea mwanaume huyo kihisia.Wanawake wanaoteswa kwenye ndoa, huwa wanajidanganya kwamba, watamudu siku moja kubadili tabia hiyo a waume zao kuwafuja. Wanajiambia kwamba, kutukanwa, kupigwa, kudhalilishwa, na matendo mengine, siyo hiari ya hao waume wao. 


Hivyo wanaamini kwamba, kuna siku watamudu kuwasaidia watoke kwenye tabia hizo. Lakini wakati mwingine wanaume hawa watesaji, huwa wanajidai kusema kwamba, wanafanya mambo hayo bila kujua sababu na kuna wakati wanasema wamelogwa.Hujawahi kuwaona wanawake wanaokwenda kwa waganga kutafuta dawa ili waume zao wasiwapige, ati kwa sababu vipigo vyao vinatokana na kuchananywa na uchawi wanaofanyiwa na wanawake zao wa nje? Mwanamke anaamini kabisa kwamba, mumewe hamjali na anamdhalilisha kwa sababu ya kulogwa!Mwanamke anaweza kujiambia kwamba, kwa sababu mume wake kuna wakati anamtendea wema, hata kama ni moja, basi anampenda na hayo mengine mabaya, yatakwisha au ni bahati mbaya. 


Mwanamke pia anaweza kufikiri kwamba, akijitahidi sana kumfurahisha mumewe, mume huyo atabadilka na kuwa na tabia nzuri. Hivyo hujipendekeza na mwanaume habadiliki na mateso yanaongezeka. Kuna wanaomudu kuishi kwenye uhusiano huu wa sababu, wamemudu kukandamiza, kupunguza ukubwa wa maumivu. Wanajiambia kwamba, wanavyotendewa siyo vibaya sana. Mwanamke anaweza kujiambia, ‘alinipiga kidogo tu, tena mara mbili kwa mwezi, kuna wanaopigwa kila siku.’ Huyu amehalalisha kipigo na mateso, hawezi kuondoka.


Kuna wanawake wanaoamini kwamba, ndoa inajengwa na kuimarishwa na mwanamke au kuvunjwa na mwanamke pia. Kuna andiko moja katika Biblia hutumiwa sana kuwatisha, linalosema, ‘Mwanamke m.p.u.m.b.a.v.u huivunja ndoa yake kwa mikono yake mwenyewe.’ Kwa hiyo wanapofikiria kuondoka, hufikiria kwamba, watu watajua na kumzonga au kumdharau kwa sababu ameshindwa kulinda ndoa. Wengine ni woga tu, kwamba, wakiondoka waume zao watawalipizia visasi au watawasumbua. kuna wakati waume wenyewe ndiyo wanaokuwa wamewatisha kwa kiwango hicho.

MWANAMKE: WATANGULIE WAMBEA MAPEMA, ILI WAKIJA KUMNONG'ONEZA AWAAMBIE 'NINAJUA'

 

Mwanamke: Watangulie wambea mapema kabisaa, ili wakija kumnong’oneza awaambie, ‘ninajua’


Hebu nikuulize wewe mwanamke. Je umewahi kumficha mumeo au mpenzi wako kitu chochote kuhusu maisha yako ya zamani au ya sasa? Je mumeo au mpenzi wako ameshawahi kukushangaza na siri ya mambo yake ya zamani? 

Inawezekana jibu likawa ndiyo au hapana, lakini kuanzia leo ningependa ujifunze jambo moja kwamba ni siri gani unatakiwa kuzitoa na ni siri gani hutakiwi kuzitoa. Usijidanganye kwamba unaweza kuficha kila siri, lakini usijiamini kwamba kwa sababu unaitwa ‘honey’ ukitoa kila siri utaweza kunyoosha uhusiano wenu, thubutuu…………….!


Lengo la kuficha jambo ni kwa ajili ya kujilinda. Unaweza kudhani kwamba, kwa kusema siri zako za zamani za masuala yako ya mapenzi utaonekana shujaa utaonekana mwadilifu au utaonekana mcha Mungu. Hapana, kuna wakati kusema kila jambo, kunakufanya ushindwe kujilinda na kumlinda mwenzi wako.


Kuna mambo ambayo huna budi kuyatoa, kama siri uliyonayo inaweza kuyumbisha mustakabali wa uhusiano wenu au kuweza kuvunja ndoa yenu. Mtaalamu wa uhusiano na mtunzi wa kitabu cha Is He Mr. Right? Mira Kirshenbaum, anasema, hata mambo ya zamani ambayo yanaweza kuleta athari katika uhusiano au maisha ya ndoa (madeni sugu, magonjwa ya kurithi, wapenzi wa zamani, tabia mbaya ambazo ulikuwa ukifanya zamani) inabidi visemwe, kutegemea tu nafasi kama vitakuja kufahamika au la. Lakini kumbuka, kama jambo linafahamika kwa zaidi ya mtu mmoja, siyo siri, litakuja kumfikia mwenzio tu.


Kuna wakati wanandoa wanaona kama wamechelewa kutoa siri na hivyo hunyamaza na baadae siri inapofichuka watu wanaanza kuchanganyikiwa. Lakini ukweli ni kutojua tu, pale unapokumbuka siri, ambayo una uhakika itafahamika kwa mwenzio, iseme, usisubiri. Tatizo la siri, ni kuwa huwa inaumiza sana. Kwa binadamu wengi kufuta uongo au usaliti siyo jambo rahisi. 


Mtu aliyefichwa siri anajiona kwamba alisalitiwa, kwa hiyo hujenga chuki kubwa. Hata kama unaona siri yako ni kuhusu jambo dogo kwako, tafadhali usimfiche mwenzio. Kama ukweli wa jambo hilo utakuja kujulikana baadae, madhara yanaweza kuwa mabaya zaidi kuliko kama ungekuwa umemwambia mapema. Sio kwamba mwenzi wako anahitaji kupata habari ili mshirikiane kutatua jambo lililo mbele yenu, lakini pia anahitaji kwa ajili ya kujua kama unamwamini.


Ipo kanuni moja kuhusu mapenzi inasema unavyozidi kutotaka kuitoa siri ndivyo unavyoiombea ijitokeze ghafla na kuanikwa hadharani. Vipi kuhusu mpenzi wako wa zamani kwamba anaweza akajitokeza ghafla ikajulikana kwa mumeo? Kama unahisi kwamba mwenzi wako anaweza kuja kupata habari za mpenzi huyo wa zamani, basi hakikisha kwamba unamweleza kabla hajatambua. 


Kujisafisha na wapenzi wako wa zamani ni jambo zuri. Bali jaribu kuwa mwangalifu, si lazima katika maelezo yako ukaanza kumsimulia mwenzio hata u.pu.u.z.i mliokuwa mkifanya wakati wa mapenzi yenu. Ni wajinga tu ndio wanaofanya hivyo.


Wenye hekima husema tu ukweli kwamba, waliwahi kuwa na uhusiano na huyu au yule na fulani na fulani. Hata kama ni kumi, wataje, ili mwenzio aamue mwenyewe, usijidanganye kwamba, hatakuja kujua. Watangulie wambea mapema kabisaa, ili wakija kumnong’oneza awaambie, ‘ninajua’


Wapo wanawake wengine huyumbisha uhusiano na weza wao au ndoa zao kwa kufukunyua mambo madogo madogo. Si vyema sana kuleta udadisi kwenye mambo madogo madogo ambayo hata hayana maana wakati mwingine. Usimsumbue mwenzio kutokana na gharama ya simu au kamera yake, hasa kama na wewe hutaki akuulize kuhusu bei ya mkoba au kidani chako……………..

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi