0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Jan 2, 2013

WANAWAKE WANABEBESHWA MENGI, NYIE ACHENI TU.....!


Mganga akaniambia mwanangu kachukuliwa msukule.....!
(Picha haihusiani na habari hii)

Mwaka 1995 nilikuwa bado naamini sana katika haya mambo ya uchawi na ushirikina. Wakati huo nilikuwa na mke na watoto wanne. Huyu mtoto mmoja, yaani huyu wa kwanza alikuwa ni mtoto wangu niliyemzaa na mwanamke mwingine, kabla sijaoa. Alikuwa ni mtoto wa kiume na wakati huo alikuwa na miaka 12, akisoma darasa la tano.

Nilifunga ndoa na mke wangu bila kumwambia kwamba, nilikuwa nina mtoto niliyezaa na mwanamke mwingine. Miaka kama mitatu baadaye akajua na ikazuka vurugu kubwa sana. Ukweli ni kwamba, nilijua nilikuwa nimekosea, lakini sikukubali kirahisi kwamba, nilikosea, badala yake nikawa najihami sana. Hata hivyo baadaye niliomba radhi, kwani mke wangu alishatishia hata kuondoka.

Baada ya kumbembeleza mke wangu alikubali mtoto huyo aishi nasi. Awali mambo yalikwenda sawa, lakini baadaye nikaona tabia za mtoto zinabadilika. Awali nilidhani zilikuwa ziko hivyo tangu kule alikotoka, lakini siku moja kaka yangu aliniambia nikague, labda mke wangu anampumbaza kwa madawa.

Awali nilidharau maelezo hayo, lakini nilianza kuhisi kuwa labda ni kweli. Kwani pamoja na kudharau nilikuwa bado nahisi uwezekano wa jambo hilo. Kwa hiyo nikawa namlinda sana mtoto. Kumbe katika kumlinda nikawa nazidi kumdekeza. Sikuwa nimejua kwamba, mama yake alikuwa amemweka mtoto huyu kwa bibi yake kwa muda mrefu na huko akadekezwa sana.Nguvu zangu zikawa kwenye kumlinda ili mke wangu asimdhuru. Kwa kweli kilikuwa ni kipindi kigumu sana. Huku unampenda mkeo, lakini unaamini anamloga mwanao na unajikuta ukiwa katikati unalea tu. Hata ule uhusiano na mke wangu haukuwa tena kama ule wa kwanza. Waingereza wanaita tention, yaani kulikuwa na hali ya wasiwasi kila mtu akisubiri chochote kitokee muda wowote.

Mtoto alizidi kuwa mkorofi na sasa nilibaini kwamba, alikuwa hata shule anatoroka. Nilianza kumlaumu mama yake na kumwambia kwamba, kama angekuwa amemzaa angefuatilia nyendo zake na kumsaidia. Mke wangu alikuwa akilia tu, na nilijua anajifaragua. Niliamini kwamba, alikuwa anamfanyia vituko ili aharibikiwe. Niliamini maneno ya kaka kwamba, mke wangu alikuwa akiogopa kwamba, mtoto huyo ndiye angerithi mali nikifa, kwani wale wengine walikuwa ni wa kike.

Mwaka 1997 akiwa darasa la saba, alianza kuvuta bangi na akawa haonekani nyumbani. Nilisikia taarifa mbaya zaidi kwamba, anatumia dawa za kulevya. Waalimu waliniita na kuniambia kwamba wamemshindwa mtoto na hawaelewi anasumbuliwa na kitu gani. ‘Ana akili sana. Kama angetulia, angefanya maajabu kabisa, sijui ni nini kinamfanya hivi.’ Nakumbuka mwalimu wake wa darasa alisema.

Nilijaribu kukaa na mtoto wangu na kuzungumza naye, baada ya adhabu ya kupiga kushindikana. Maana nilipoona kumdekeza kunamharibu zaidi nikaamua kumcharaza viboko. Lakini hayakuzaliwa matunda. Hata hivyo, kutoroka shule kulipungua kidogo na akawa anaonekana nyumbani ingawa kwa muda mbaya. Kuna wakati anarudi nyumbani saa tatu usiku, akiulizwa anasema, ‘usafiri,’ wakati shule haizidi umbali wa kilomita mbili kutoka nyumbani.

Siku moja Agosti mwaka 1997 alitoroka nyumbanin bila kuchukua nguo zake wala chochote. Ajabu ni kwamba, mimi ndiye niliyekuwa wa kwanza kuamka na kufungua mlango mkubwa. Nilipoingia chumbani kwake kumwamsha ili ajiandae kwenda shuleni, sikumkuta. Nilishangaa, kwa sababu alilala ndani na kama ni kutoka usiku, mlango ungekuwa wazi au ungefungwa kwa nje.

Siku hiyo sikwenda kazini, bali nilienda kituo cha Urafiki na kuripoti. Niliambiwa kwamba, kupotea mtu ni hadi zipite saa 24, hivyo niripoti kesho yake kama sijampata. Nilirudi nyumbani na kumwambia mke wangu aseme alipo mtoto. Nakumbuka mshangao wake usoni mwake. Aliniuliza nina maana gani. Nilimwambia mtoto hawezi kupotea kama kuku. Nilitoka na kuelekea kwa kaka yangu Kijitonyama. Nilimweleza kilichotokea. Aliniambia, ‘Nilikwambia ndugu yangu. Huyu mtoto naamini kabisa kachukuliwa msukule, kafichwa na mama yake wa kambo. Mimi nitakupeleka mahali, utajua kila kitu.’ Alisema.

Halafu aliongeza, ‘usimwambie mkeo lolote, maana atazuia juhudi zetu.’ Nilikubali ingawa nilikuwa bado na maswali kama ninachofanya ni sahihi. Nilikubali hata hivyo. Nilienda kazini na kuomba ruhusa, nikisema mwanangu anaumwa sana. Nilipewa ruhusa ya wiki moja. Tuliondoka na kaka yangu asubuhi, nikimwambia mke wangu naenda Morogoro (Kwa mama wa mtoto yule) kuona kama kakimbilia huko. Mke wangu alikubali na hakuwa na amani. Kukosa kwake amani nilijua ni kutokana na ukweli kwamba, yeye ndiye aliyekuwa amehusika na kupotea kwa mtoto. Kaka yangu alinipeleka kwenye kijiji kimoja kinachoitwa Kwa Msisi huko Handeni, Tanga. Kuna mganga ambaye nisingependa kumtaja jina, ambaye huyo ilidaiwa na huenda inadaiwa kwamba, kwa kurudisha watu waliochukuliwa msukule ndiyo kazi yake.

Tulipofika tulipokewa kama wateja na kutajiwa shida yetu. ‘Mmepotelewa, siyo mali wala kitu gani, bali chenye damu.’ Aliposemam hivyo yule mganga niliogopa sana. Ni kweli alikuwa mganga. Jioni ya siku hiyo tulianza shughuli kwa kwenda makabutini na baadae kurudi ambapo alichinjwa kuku mwekundu. Ilikuwa kama saa sita usiku. Mganga yule alisema mwanangu, yumo ndani ya nyumba yetu anafanyishwa kazi.

Nilipouliza ni nani anamfanyisha kazi, alisema kuna siku nitamjua. Aliniambia nitoe shilingi 50,000 na akanipa dawa za kuweka mle ndani. Alisema kuna siku mtoto huyo atajitokeza, hautazidi mwezi mmoja, lakini atakuwa anatisha. Alisema akijitokeza tumshike na kumfunga kamba na kumpeleka kwa mganga. Tuliondoka kule Kwa Msisi nikiwa nimesawajika kabisa. Nilijua mke wangu alikuwa fisadi mkubwa. Niliporudi sikuzungumza naye habari ya mtoto, hata aliponiuliza kilichotokea huko Morogoro.

Nilimwambia, ‘tulia tu, mnafiki atapatikana sasa hivi.’ Hakuelewa, ingawa alionekana kunikagua kwa wasiwasi sana. Nikawa nafanya zile dawa nilizoambiwa. Nilimaliza wiki nzima ya dawa. Mwezi ulipita, miezi miwili hadi mitatu, hakuna mtoto kujitokeza. Wakati huo wote nilikuwa nalala kwa machale sana. Nikisikia mchakato kidogo, naamka na kwenda kuangalia, nadhani ni mwanangu. Hatimaye nikarudi kwa kaka na kumwambia, nadhani mganga yule ameshindwa. Kaka yangu alikuwa mshirikina kuliko mimi, kwani alinitajia mganga mwingine ambaye aliniambia anaishi Ikwiriri, Rufiji. Niliomba likizo kabisa kazini ili nijue mwisho wa jeuri ya mke wangu. Kumbuka wakati huo nilikuwa sina kabisa mawasiliano na mke wangu. Niliamini ni mchawi mbaya sana.

Tuliondoka na kaka yangu hadi kwa huyo mganga. Huko nako niliambiwa mwanangu yu mzima, bali amefichwa kwenye nyumba moja yenye Mghahawa hapo karibu na kazi yake ni kuita wateja. Yaani anawaita wateja kimizungu na hao wateja wanajikuta wakiingia mghahawani bila kujua ni kwa nini. Nilitoa shilingi 100,000 kwa ajili ya kutengenezewa dawa za kumfanya afukuze wateja badala ya kuwaita, ili aliyemchukua amrudishe.

Nilipouliza ni nani aliyemchukua mtoto wangu kumpeleka huko, mganga alisema, ni mtu wa karibu yangu sana, lakini hakumtaja. Hasira dhidi ya mke wangu ilizidi. Kwa kweli, nilirudi nyumbani, hatua ya kwanza ilikuwa ni kumwomba mke wangu aende kwao kwanza hadi nitakapopunguza hasira zangu. Alipouliza sababu, nilimpiga sana. Ilikuwa ni mara ya kwanza kumpiga.

Aliniuliza kama nimelogwa hadi nikachanganyikiwa. Hapo ndipo nilipomwambia ukweli, kuhusu kumchukua mtoto na kumfanyia mazingira. Alishikwa na butwaa na aliingia ndani mara moja na kuchukua kilicho chake. Baadae nilijua kwamba alikwenda kwa kaka yake aliyekuwa akiishi Sinza. Mimi nilianza uchunguzi kwenye ule mghahawa. Ajabu sikuona wateja wengi sana wakiingia mle. Waliingia wateja wa idadi ya kawaida tu.

Mwaka 1998 nikiwa naangalia TV kwenye taarifa ya habari niliona vijana wanne ambao walikuwa wameshikiliwa na Polisi. Walikuwa ni vijana wanaojihusisha na kuuza bangi na uporaji. Mmoja kati ya vijana wale alikuwa ni mwanangu kwa jina na sura.

Asubuhi saa 12 nilikuwa kituo kikuu cha Polisi. Kwa kweli sikuamini macho yangu, kwani alikuwa ni yeye. Niliruhusiwa kumwona na kumwekea dhamana kwenye saa saba hivi. Nilirudi nyumbani nikiwa nimeshukwa na uso.

Nilipomuuliza alipokuwa, alisema alikimbilia Zanzibar kwa rafiki yake na badaye kurejea Dar na akawa anaishi Kawe.

Aibu, fadhaa na jitimai vilinivaa vibaya. Nilijiuliza kuhusu tuhuma nilizomshushia mke wangu na aibu kubwa ambayo ningeipata kwa wale wote ambao walijua kilichoendelea. Nilimwambia mwanangu kama anataka kuishi name abadilike, kama hawezi akatafute baba mwingine. Bahati mbaya hata hivyo, katika kesi yake ile ya kuuza bangi alihukumiwa kwenda jela miaka mitatu. Aliugua kifua kikuu akiwa jela na mwaka 2000 alifariki.

Nilimrudisha mke wangu baada ya kazi kubwa sana. Nilisemwa na ndugu na wazazi wake kama mtoto. Kuanzia wakati ule hadi leo ukinitajia ramli au mganga wa kutoa misukule au televisheni ya asili au wachawi, naweza kukung’oa meno. Nauliza ni wangapi wanadanganywa kama mimi……..?

Hii habari hainihusu mimi.

2 comments:
Andika Maoni Maoni
  1. huyo jamaa ni mpumbavu uchawi upo ndio lakini alitakiwa amuangalie mwanae kwanza kabla ya kuyafatlia hayo mambo

    ReplyDelete
  2. jamani! amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu kuwa ngao au kinga ya maisha yake

    ReplyDelete

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi