0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Jun 9, 2011

AKAJISIFU KOROGWE KAMA YEYE NI TAJIRI



Ingawa tukio hili lilitokea takribani miongo minne iliyopita lakini ni tukio ambalo liliacha simulizi katika jiji la Dar Es Salaam na vitongoji vyake.


Tukio hili lilitokea mnamo July 23, 1977 majira ya saa tatu na dakika arobaini na tano za asubuhi katika mtaa wa Nkrumah kwenye duka la DARTEX ambapo majambazi wawili waliokuja kujulikana baadae kwa majina ya Aidan John Alfonce Mweri ambae ndie aliyekuwa mshitakiwa wa kwanza katika kesi hii na mwenzie John Joseph Tarimo aliyekuwa mshitakiwa wa pili walivamia gari la DARTEX lililokuwa lisafirishe fedha kuzipeleka benki.


Majamabzi hao ambao inasemekana walikuwa wanafahamu mpango huo wa kupeleka fedha benki yalikuwa yamejipanga jirani kabisa na eneo la duka hilo la DARTEX huku wakiwa na silaha zao.


Fedha hizo zilikuwa zipelekwe na watu watatu waliotajwa kwa jina moja moja ambao ni Bi Sanga ambae alikuwa ni mhasibu wa DARTEX na ndie aliyekuwa amebeba mkoba wenye fedha kiasi cha shilingi 627,603.45 na hudi zenye thamani ya shilingi 125,192.35 ambazo zilitokana na mauzo ya jana yake katika duka hilo, wengine walikuwa ni Mwakalasa askari polisi na Gongolo ambae alikuwa ni mwanajeshi, wote walikuwa wanamsindikiza Bi Sanga kupeleka fedha hizo benki.


Wakati wakijiandaa kupanda gari dogo lililokuwa limeegeshwa nje ya duka hilo ndipo katika hali ya kushtukiza majambazi hao wakafytua risasi hewani mara kadhaa na kusababisha hali katika eneo lile kuwa ya kuogofya na watu wote waliokuwa katika eneo lile walikumbwa na mshtuko kiasi cha kuanza kukimbia hovyo huku na huko kwa kihoro.


Katika hali ya kuzuia uporaji ule askari polisi Mwakalasa alanza kurushiana risasi na jambazi mmoja, lakini kwa bahati mbaya akajeruhiwa na risasi tumboni na lakini hata hivyo aliendelea kukabiliana na jambazi yule kwa kurushiana nae risasi mpaka akamjeruhi katika mkono wake wa kushoto na hivyo kudondosha bastola yake na kuanza kukimbia kutoka katika eneo la tukio ili kusalimisha maisha yake.


Nae Mhasibu wa DARTEX Bi Sanga akiwa bado amekumbwa na mshituko asijue la kufanya alishitukia akinyang’anywa mkoba wenye fedha na jambazi mwingine aliyekuja kujulikana baadae kwa jina la Aidan John Alfonce Mweri, hiyo ilikuwa ni baada ya kumtisha kwa bastola na kutokomea nao kusikojulikana.


Jambazi mwingine John Joseph Tarimo alionekana akikimbia kutoka katika eneo la tukio na kuingia katika jengo moja la ghorofa ambalo lilikuwa limepangishwa na mhindi.


Hata hivyo baadae Jambazi huyo alikamatwa kwa ushirikiano wa raia wema na Polisi na alionekana akiwa anavuja damu katika mkono wake kuashiria kuwa alikuwa amejeruhiwa kwa risasi kutokana na mapigano yale ya kurushiana risasi na Polisi.


Baadae ilikuja kubainika kwamba baada ya kufanikiwa kukimbia na mkoba wenye fedha Mweri alikwenda Korogwe na kununua nyumba mbili.


Hata hivyo wakati akiwa Korogwe ilizuka minong’ono katika mji huo wa Korogwe na vitongoji vyake kwamba Mweri alikuwa akijigamba kwamba ana fedha nyingi sana.


Nao Polisi katika mji wa Korogwe wakaisikia minong’ono hiyo, hivyo wakaanza kumtilia mashaka mtuhumiwa huyo.


Mnamo November 5, 1977 polisi walivamia nyumbani kwa Mweri na kufanya upekuzi ambapo walipata kiasi cha shilingi 48,705.50 zikiwa katika mfuko wa karatasi. Hata hivyo upekuzi huo haukuwa na uhusiano na wizi wa DARTEX.


Baadae Mweri alikamatwa na kupelekwa kituoni kwa mahojiano zaidi.


Ikumbukwe kwamba katika miaka hiyo ya 70 mtu kukutwa na kiasi kikubwa cha fedha bila ya maelezo mazuri ya namna ulivyozipata fedha hizo lilikuwa ni kosa kisheria.


Lakini hata hivyo wakati Mweri akiendelea kuhojiwa na Polisi mjini Korogwe, polisi wakadokezwa kwamba mtuhumiwa huyo anatafutwa na Polisi wa jijini Dar akihusishwa na tukio la uporaji uliotokea katika duka la DARTEX, hivyo Polisi wa mjini Korogwe wakamrejesha jijini Dar.


Hatimaye alipofikishwa jijini Dar akaunganishwa na mwenzie na kusomewa mashitaka ya unyang’anyi wa kutumia silaha kosa ambalo linaangukia katika vifungu vya sheria 285 na 286 vya makosa ya jinai na kosa lingine likiwa ni la kumiliki silaha kinyume cha sheria, kosa ambalo linaangukia katika kifungu cha 8 (1) cha sheria ya makosa ya usalama wa taifa ya mwaka 1970.


Washtakiwa wote wawili walikana mashitaka yao ambapo upande wa mashitaka ulileta mashahidi wake.


Miongoni mwa mashahidi walioitwa walikuwa ni Chiku Nasibu ambae alikuwa ni shahidi wa pili katika kesi hiyo na Zainabu Ali ambae alikuwa ni shahidi wa nne, ambapo wote wawili walikuwa katika eneo la tukio siku hiyo uporaji ulipotokea.


Akitoa ushahidi wake Shahidi wa nne Zainab Ali aliiambia mahakama kuwa yeye alikuwa ni mteja wa muda mrefu wa duka hilo la DARTEX.


Akisimulia zaidi shahidi huyo aliieleza mahakama hiyo kwamba siku hiyo ya tukio majira ya asubuhi alikwenda dukani hapo kama kawaida yake kununua bidhaa huku akiwa ameandamana na mwenzie shahidi wa pili Chiku Nasibu.


Akiwa pale dukani kama nasibu vile alimuona mshitakiwa wa kwanza Mweri akiwa amesimama nje ya duka, hata hivyo shahidi huyo alibainisha kwamba kwa njia moja ama nyingine kitendo cha kumuona mtuhumiwa yule mahali pale kilimtia mashaka.


Shahidi huyo aliendelea kusema kwamba mtuhumiwa huyo alikuwa ameegemea kwenye gari la kusambaza vifaa vya masijala (Stationary), huku akionekana kama anasoma gazeti au alikuwa anajenga mazingira ya kuonekana kuwa alikuwa anasoma gazeti.


Huku akimnyooshea kidole mtuhumiwa, Zainabu alitaka kumjulisha jambo shahidi wa pili Chiku kuhusiana na mtuhumiwa wa kwanza Mweri ndipo ghafla kwa mshituko wakasikia mlio wa risasi iliyofyatuliwa na mtu mwingine aliyekuwa katika eneo hilo la tukio, huku akindelea kushangaa alimuona mshitakiwa wa kwanza akichomoa bastola yake na kumfuata mhasibu Bi Sanga na kumpora mkoba wenye fedha kwa kumtisha na bastola yake.


Huku akikimbia na fedha hizo alimuona mshitakiwa huyo akirusha risasi, Pia aliona Polisi akirushiana risasi na mtu mwingine ambae alikuwa na sura ngeni kwake.


Akijibu mojawapo ya maswali aliyoulizwa na mahakama, Zainab alisema kwamba yeye anaishi mtaa Bungoni jijini Dar, na nyumba yake iko mkabala na ya mshitakiwa wa kwanza na ametokea kumfahamu mshitakiwa huyo kwa zaidi ya mwaka mmoja.


Nae mshitakiwa wa pili Chiku ushahidi wake haukutofautiana na wa shahidi wa nne Zainab.


Kwa mujibu wa maelezo yake shahidi huyo alikiri kujulishwa na shahidi wa nne kuhusu kuwepo kwa mshitakiwa wa kwanza katika eneo la tukio, pia alisikia mlio wa risasi ghafla.


Shahidi huyo alimuona polisi akitokwa na damu baada ya kupigwa risasi na pia alimuona mshitakiwa wa kwanza akimnyang’anya mhasibu Bi Sanga mkoba wenye fedha.


Ushahidi mwingine uliotolewa mahakamni hapo ulikuwa ni dhidi ya mshitakiwa wa pili John Joseph Tarimo.


Ushahidi dhidi yake ulitolewa na mashahidi watatu ambao ni aliyekuwa shahidi wa kwanza katika kesi hiyo Mwakalasa, shahidi wa sita Joseph na shahidi wa 14 Songolo.


Shahidi wa kwanza Mwakalasa alikuwa ni Polisi mwenye cheo cha Sajenti Meja na alikuwa amepangiwa jukumu la kusindikiza fedha za DARTEX kupelekwa benki.


Akitoa ushahidi wake mahakamani hapo Mwakilasa aliieleza mahakama kwamba wakiwa wanajiandaa kupanda gari ambalo walikuwa ndilo walitumie kupelekea fedha benki alistukia anapigwa na risasi tumboni.


Mara akamuona mshitakiwa wa pili akiwa ameshika Bastola katika mkono wake wa kulia na kuanza kumfokea “Askari Kimbia”, lakini kwa ujasiri kwa kutumia bunduki yake aina ya Sub-Machine Gun alirusha risasi ambayo ilimjeruhi mshitakiwa huyo wa pili, hivyo akaanza kukimbia kutoka katika katika eneo la tukio huku akirusha risasi ambayo ilimjeruhi raia mmoja mwenye asili ya kiasia ambae alikuwa kwenye eneo la tukio.


Mwakalasa alimkimbiza mshitakiwa huyo na kumpiga risasi katika mkono wake wa kushoto ambapo alidondosha Bastola ambayo alikuwa ameishika mara baada ya kupigwa risasi hiyo.


Shahidi huyo aliiokota bastola hiyo ambayo ilitumika mahakamini kama kidhibiti cha kwanza.


Mara baada ya kuokota bastola hiyo aliendelea kumkimbiza mshitakiwa huyo ambapo mbio hizo ziliishia katika ghorofa ya tatu kwenye jengo lingine lililojulikana kwa jina la Kulsum Mansion alilokuwa akiishi raia mwingine mwenye asili ya kiasia aliyejulikana kwa jina la Lakhani ambae alikuja kuwa shahidi wa 15 katika kesi hiyo.


Shahidi huyo aliukuta mlango wa katika ghorofa hiyo ukiwa umefungwa hivyo aliona nivyema akimbilie hospitali kutibiwa jeraha la risasi aliyopigwa na kuamua kumuacha shahidi wa 6 aliyejulikana kwa jina la Joseph nje ya jengo hilo ili kumlinda mshitakiwa asitoroke kabla ya kutiwa mbaroni, hivyo alimkabidhi silaha aliyokuwa nayo ambayo ilikuwa ni Sub Machine Gun pamoja na Bastola aliyoidondosha mshitakiwa.


Shahidi huyo aliithibitishia mahakama kwamba ana uhakika kabisa kwamba mtu ailyerushiana nae risasi na aliyedondosha bastola ni mshitakiwa wa pili John Joseph Tarimo.


Shahidi aliyefuatia kutoa ushahidi wake dhidi ya mshtakiwa alikuwa ni shahidi wa sita katika kesi hiyo aliyejulikana kwa jina la Joseph.


Kwa upande wake Joseph ambaye alikuwa ni askari Polisi aliyekuwa na cheo cha Coplo aliiambia mahakama kwamba siku ya tukio alikuwa katika Hoteli ya kitalii ya Rex, ndipo ghafla akasikia milio ya risasi ikirindima kutokea upande lilipo duka la DARTEX. Shahidi huyo alikimbilia katika eneo la tukio haraka ili kutoa msaada, alipokaribia tu akamuona shahidi wa kwanza Mwakalasa akimkimbiza mshitakiwa wa pili huku akiwa ameshikilia bunduki aina ya Sub Machine Gun pamoja na bastola, na ndipo akaamua kumsaidia kumkimbiza mshitakiwa huyo wa pili ambapo alikuja kumkuta mwakalasa akiwa nje ya mlango katika ghorofa hilo ambao ulikuwa umefungwa kwa ndani.


Ndipo Mwakalasa akamuomba ampokee silaha na aendelee kumfuatiali mshitakiwa kwani hali yake haikuwa nzuri kutokana na kupigwa risasi tumboni hivyo alitaka kukimbilia hospitali kwa matibabu.


Shahidi huyo aliendelea kuielezea mahakama kwamba alipokea Bunduki na Bastola kutoka kwa Mwakalasa kisha akamuamrisha mshitakiwa afungue mlango kwa usalama wake kitu ambacho hakutii, hivyo akaamua kupiga risasi kwenye mlango, ndipo mshitakiwa huyo akafungua mlango na kujisalimisha.


Baada ya kutiwa mbaroni, baadae alikimbizwa hospitalini kwa matibabu kutokana na kujeruhiwa kwa risasi.


Shahidi wa mwisho kutoa ushahidi wake dhidi ya mshitakiwa wa pili ni mwanajeshi Songolo ambaye alikuwa ni shahidi wa 14 aliyekuwa akilinda katika duka la DARTEX.


Kwa ujumla ushahidi wake haukutofautiana sana na ushahidi wa Mwakalasa na wa Joseph.


Katika utetezi wake mshitakiwa wa kwanza Aidan John Alfonce Mweri ambaye alijitambulisha pale mahakamni kama mfanyabiashara wa mbao alikanusha kabisa kushiriki katika uporaji ule.


Mshitakiwa hiyo alikanusha kuwepo katika eneo la tukio na wala kuhusika na uporaji uliotokea.


Akizungumzia ushahidi uliotolewa dhidi yake na shahidi wa pili Chiku Nasibu na shahidi wa nne Zainabu Ali Mshitakiwa huyo alidai kwamba mashahidi hao ni waongo kabisa.


Mweri alidai kwamba mashahidi hao walikuja kutoa ushahidi huo dhidi yake kwa sababu ya chuki binafsi alizokuwa nazo shahidi wa nne dhidi yake.


Mweri aliendendelea kuieleza mahakama kwamba anakumbuka mwanzoni mwa mwaka 1977, akiwa anaendesha gari lake ilibaki kidogo tu amgonge mtoto wa shahidi wa nne Zainab Ali ambae alikatisha barabarani ghafla bila kuchukuwa tahadhari, basi kuanzia wakati huo shahidi huyo alijenga uhasama mkubwa sana na yeye.


Mshitakiwa huyo aliiomba mahakama hiyo ipuuze ushahidi wa mashahidi hao wawili kwa sababu hakuna shahidi mwingine aliyetoa ushahidi dhidi yake.


Akizungumzia kuhusu kumiliki nyumba mbili Korogwe, mshitakiwa huyo alidai kuwa nyumba hizo ni za familia yao na yeye aliteuliwa kuwa msimamizi wa nyumba hizo.


Zamu ya mshitakiwa wa pili John Joseph Tarimo ilipofika mshitakiwa huyo alikanusha madai ya kwamba yeye ni mmojawapo wa wahusika wa tukio la uporaji katika duka la DARTEX na wala sio mmiliki wa bastola iliyoletwa pale mahakamani kama kidhibiti.


Mshitakiwa huyo aliieleza mahakama hiyo kwamba yeye alikuwa jirani au katika eneo la tukio wakati milio ya risasi iliposikika, kwa hiyo madai ya kuwepo kwake katika eneo la tukio wakati uporaji huo unatokea hawezi kuupinga.


Akiendelea kusimulia zaidi kuhusu tukio hilo mshitakiwa huyo alidai kwamba yeye ni mchuuzi wa samaki kutoka Nyumba ya Mungu mkoani Kilimanjaro, hivyo mnamo Julai 21, 1977 alileta samaki jijini Dar ili kuziuza, ambapo alipomaliza kuuza samaki wake katika soko la kariakoo aliamua kwenda kufanya manunuzi ya bidhaa mbalimbali siku ya Julai 23, 1977.


Katika mizunguko yake alijikuta akiwa mtaa wa Nkurumah karibu na duka la DARTEX na ndipo aliposikia milio ya risasi na kuona watu wakikimbia ovyo.


Wakati watu wakiendelea kukimbia aliona baadhi ya watu wakiwa wameshika bunduki na baada ya kuona hali katika eneo hilo si shwari nae akaamua kukimbia ili kusalimisha maisha yake.


Mshitakiwa huyo aliendelea kuieleza mahakama hiyo kwamba, wakati anakimbia alijikuta akianguka na kuumia mkono wake wa kushoto lakini kwa bahati nzuri aliweza kuamka na kuendelea kukimbia,


Hata hivyo mshitakiwa huyo alibainisha kwamba wakati akiendelea kukimbia akashitukia anapigwa risasi, lakini alimudu kukimbia mpaka kwenye ghorofa lilikuwa jirani na kisha akapoteza fahamu, aliporudiwa na fahamu siku iliyofuata alijikuta akiwa amelazwa hospitalini.


Kesho yake aliruhusiwa kutoka hospitalini na alichukuliwa na polisi hadi kituo cha kati cha Polisi na kuwekwa ndani.


Mnamo Agost 25, 1977 alipatwa na mshituko kusikia akisomewa mashitaka uporaji wa kutumia silaha dhidi yake.


Shahidi wa mshitakiwa wa pili Silas Lucas Mbwambo waliwahi kufungwa pamoja katika gereza la ukonga.


Wote wawili walikuwa mahabusu katika gereza la Keko kipindi cha nyuma .


Shahidi huyo akitoa ushahidi wake wa kumtetea mshitakiwa wa pili alidai kwamba mtu aliyekuwa akirushiana risasi na shahidi wa kwanza polisi Mwakalasa na aliyemjeruhi raia mwenye asili ya kiasia alikuwa ni mtu aliyemtaja kwa jina la Juma Shabani na sio mshitakiwa wa pili.


Shahidi huyo aliendelea kudai kwamba alimuona Juma Shabani akitoroka kutoka katika eneo la tukio kwa gari huku akiendesha kwa mwendo wa kasi.


Kesi hiyo ya jinai namba 1207 ya mwaka 1977 ilisikilizwa na hakimu L F Musiba ilifikia tamati yake mnamo November 5, 1979 na washitakiwa walipatikana na hatia.


Hata hivyo washitakiwa hawakuridhishwa na uamuzi wa mahakam ya kuwatia hatiani hivyo walikata rufaa katika mahakamaa kuu.


Rufaa hiyo iliyosikilizwa na Jaji D P Mapigano na katika uamuzi wa mahakama kuu rufaa hiyo ilitupiliwa mbali mara baada ya kupitia upya ushahidi wa pande zote mbili.


Hivyo mahakama kuu iliwahukumu washitakiwa wote wawili kifungo cha miaka 10 jela kwa kosa la kwanza na kifungo cha mwaka mmoja kwa kosa la pili, na adhabu zote mbili zitatumikiwa kwa pamoja, pia washitakiwa hao walitakiwa kurejesha fedha walizoiba DARTEX baada ya kumaliza kutumikia vifungo vyao.


Akihitimisha kusoma hukumu hiyo kwa maneno yake mwenyewe Jaji Mapigano alisema “Kosa walilolifanya washitakiwa ni kubwa lisiloweza kuvumilika katika jamii, hivyo kama alivyowahi kusema waziri wa mambo ya ndani kuwa matukio ya ujamabazi wa kutumia silaha yamefikia katika kiwango cha kutisha nchini hivyo washitakiwa hawa watapewa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine” alimalizia kusema Jaji Mapigano kabla ya kutoa hukumu hiyo.



3 comments:
Andika Maoni Maoni
  1. Ni kesi ya zamani kweli lakini inafundisha. nilikuwa nawaza, kumbe zamani ilikuwa majambazi hawauawi hovyo kama ilivyo sasa hivi! nimeshangaa kwamba yule Askari alimjeruhi Jambazi kw akumpiga risasi ya mkono ambao ulishika bastola, lengo ikiwa ni kumvunja nguvu na kumkamata na kuhakikisha anafikishwa kwenye vyombo vya sheria,........

    Lakini siku hizi....thubutuuu... utasikia tu. majambazi idadi fulani wameuawa mahali fulani, katika mampambano na Polisi....

    Nawaza tu....

    ReplyDelete
  2. ''....Kosa walilolifanya washitakiwa ni kubwa lisiloweza kuvumilika katika jamii, hivyo kama alivyowahi kusema waziri wa mambo ya ndani kuwa matukio ya ujamabazi wa kutumia silaha yamefikia katika kiwango cha kutisha nchini hivyo washitakiwa hawa watapewa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine...''
    Kweli inakuwa fundisho?

    ReplyDelete

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi