0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Mar 4, 2009

SIFA YA DAKIKA YAWEZA KUBADILI KABISA MAISHA

Sifa ya dakika moja yaweza kufanya maajabu
Leo ningependa kuwasimulia kisa hiki ambacho kiliwahi kuandikwa katika Gazeti la Jitambue. Naamini kuna kitu tutajifunza kutokana na kisa hiki ingawa kiliandikwa zamani kidogo.

Akiwa chuoni bado mwanafunzi wa kozi ya uhandisi Selemani Mtansi alipata kazi ya muda wakati wa likizo yake. Alipata kazi hii kwenye kiwanda kimoja cha kukata magogo na kusafirisha nje kilichoko huko morogoro. Siku moja msimamizi mkuu wa kiwanda hicho alipata dharura iliyomfanya asafiri kwa siku tatu.

Kutokana na kumwamini Sulemani alimuachia madaraka ya kuwasimamia vibarua kiwandani hapo. Labda hii ilitokana na kwamba Sulemani alikuwa mwenye elimu ya juu ukiwalinganisha na wengine waliokuwa kwenye nafasi ya kuweza kuachiwa madaraka. Lakini pia Selemani alikuwa ni mwenye nguvu.

Kabla msimamizi hajaondoka Selemani alimuuliza, ‘Je kama atatokea kibarua kunibishia au kukataa amri zangu nifanyeje, kwa sababu kama unavyojua kuna vibarua wakorofi sana hapa kwa sababu mbalimbali?’ lakini zaidi pengine alikuwa amelenga kibarua mmoja aliyekuwa akiitwa Popii ambaye alikuwa ni mtu wa kulalamika na kulaani huku akifanya usumbufu wa hapa na pale na kukera sana.

‘fukuza kazi tu, hakuna haja ya kumchekea mjinga’. Msimamizi alimjibu Selemani.
Hata hivyo baada ya kufikiri kidogo msimamizi alimwambia ‘nadhani unafikiria kumtimua Popii kama atakosa nidhamu, hilo bila shaka ni lazima nikiri kuwa litanikera kwani huyu kijana ni wa kuaminika sana kwa kadri ninavyo fahamu kazi hii ya magogo ambayo nimeifanya kwa miaka ishirini hadi sasa’.

Halafu aliendelea, ‘Popii ni mkorofi na anamchukia karibu kila mtu na karibu kila kitu. Lakini kama umechunguza tangu uje hapa yeye ndiye wa kwanza kuja na wa mwisho kuondoka. Hakujawahi kutokea ajali kwa miaka sita sasa tangu amekuwa hapa, na wafanyakazi wote wanakiri kwamba bila yeye ajali nyingi zingetokea. Ana uwezo wa kunusa ajali kwa njia inayowashangaza wengine’.

Selemani alianza usimamizi rasmi siku iliyofuata. Asubuhi hiyo hiyo alimfuata Popii na kuanza kuzungumza naye. ‘Popii unajua mimi ndiye msimamizi kwa leo na siku mbili zijazo?’ Popii aligunia kama vile amepigwa na kitu chenye kutia maumivu. ‘Ukweli ningekufukuza kazi muda wowote ambapo tungekwaruzana kidogo tu, lakini sitafanya hivyo’. Alimwambia Popii na kumweleza kuhusu msimamizi mkuu alivyomsifu.

Selemani alipomaliza kuzungumza Popii aliweka chini msumeno aliokuwa ameushika na kuhisi machozi yanamlengalenga na baadae kumdondoka kabisa. ‘ kwa nini bosi hakuniambia miaka sita iliyopita?’ alimuuliza akimwacha Selemani akiwa ameduwaa.

Vibarua, wasimamizi wengine pamoja na Selemani walishangaa sana kwani baadae siku ile, Popii alifanya kazi katika kiwango cha juu na cha kutisha, kiwango mara mbili ya kile alichokuwa akisifiwa nacho. Siyo kufanya kazi tu peke yake bali alitabasamu akiwa kazini kwa mara ya kwanza.

‘Nitamsimulia mke wangu leo kwamba wewe ni msimamizi wa kwanza kuniambia kuwa ni mchapa kazi, sijawahi kuambiwa hivyo na yeyote kwa miaka sita niliyofanya kazi hapa, wewe ni wa kwanza na hivyo najiona kama nimezaliwa upya’ Popii alimwambia Selemani jioni ile.

Baada ya likizo Selemani alirudi chuoni kumalizia masomo yake. Miaka minne baadae alibahatika kukutana na Popii Tanga. Alishangaa pale Popii alipomjulisha kuwa alikuwa meneja kwenye kiwanda kama kile cha morogoro lakini ambacho kiko Muheza mkoani Tanga. Kutoka kibarua mkorofi hadi meneja katika kipindi cha miaka minne ni lazima mtu ashangae.

Selemani hakusita kumuuliza Popii siri ya mafanikio yake kwa kipindi hicho kifupi. ‘Kama ingekuwa siyo yale mazungumzo yako ya dakika mbili kwa siku ile asubuhi kule morogoro ni lazima kuna siku ningeuwa mtu au kujiua mwenyewe napengine vyote. Zile dakika mbili tulizo simama nawe ukanisifia ndizo zilizobadilisha maisha yangu. Siri ya mafanikio yangu ni zile dakika mbili na kukubali kwangu kubadilika. Alisema kwa kujiamini.

Mameneja au wasimamizi wazuri wanajua umuhimu wa kuchukua angalau dakika moja kumwelezea mtumishi au aliye chini yake namna anavyofanya kazi vizuri. Unadhani ni tofauti zipi inaweza kupatikana kwa dakika moja ya kumthibitisha mtu kwa ubora wake kwenye uhusiano wowote? Ni tofauti kubwa bila shaka.

Dakika moja au mbili tu! Je umeshawahi kutumia dakika moja kumshukuru mtu kwa utendaji wake au kwa chochote ambacho amekifanya hata kama ni kidogo? Kama bado, kumbuka kwamba unampotezea mtu huyo nafasi kubwa sana ya kubadilika, nafasi ya kumfanya naye ajue au kugundua kwamba anathaminiwa na hivyo kumfanya kutoka kwenye maisha ya ‘bora-liende’. Kama aliyokuwa nayo Popii hapo kabla.

Dakika moja ya kumfahamisha mtu kwamba alichofanya ni kikubwa na kizuri inaweza kubadili kabisa maisha ya mtu huyo. Popii alimuuliza Selemani kwamba ni kwa nini msimamizi mkuu alishindwa kumwambia maneno yale kwa miaka sita aliyokuwa akifanya kazi pale kiwandani? Kushindwa kumwambia kulimfanya kudhani kwamba hana faida na yeye ni mkorofi tu, hivyo akawa anaishi hivyo, akaamua hayo yawe maisha yake.

Watoto wetu, wapenzi wetu, watumishi wetu, jirani zetu (yaani watu tunaokutana nao popote hata kwa dakika moja) wanastahili hata dakika hiyo moja ya kupongezwa kwa kazi nzuri waliyofanya, kwani kuambiwa huko kunaweza kumfanya kuondoka kwenye udhaifu alionao na kuanza kufanya mazuri mengi kuliko mtu anavyoweza kutarajia.

Ni ukatili na kutojali wengine pale tunapoona kabisa mtu fulani anastahili sifa fulani tukanyamaza na kumsifia kimoyomoyo tu. Kwa nini mtu anapokosea tunapenda kumkosoa? Lakini lazima ufahamu kuwa kukosoa huko hakusaidii lolote zaidi ya kuzidi kumpeleka pabaya wakati kumsifu kunaweza kumbadili kabisa.

1 comment:
Andika Maoni Maoni
  1. kweli kabisa hata kwa wazazi wetu bwana. nakumbuka kumpigia simu mama mmoja niliyekuwa na uhusiano naye, yule mama alinii ta 'mwanangu mpenddwa'

    nilishindwa kuongea, nikapigwa na butwaa, nikatokwa na machozi ya furaha. kumbe na mimi huwa napendwa? nilijiuliza.

    ReplyDelete

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi