0715 72 92 92

SHABAN KALUSE

Kwa Matangazo na mambo mbalimbali & Wasiliana Nami

http://www.serenahotels.com/serenadaressalaam/default-en.html

Nov 22, 2009

NI MAMA! SEHEMU YA MWISHO

Ø Amtazama mtoto na kusema bila mabadiliko atakufa mtu
Ø Awabadilikia mume na binamu zake dakika chache baada ya ndoa
Ø Atangaza kwa mtoto kwamba yeye ni mama aliyekufa zamani amerudi

Mwaka ukakatika na wenzangu wa lifunga na kufungua shule wakaingia darasa jipya, mwaka 1973. Nilitakiwa niwe darasa la tano, lakini badala yake nilishaanza kuzoea maisha ya mitaani. Mwaka huo huo, Februari ndipo ambapo baba aliamua kuoa. Nilisikia akiwaambia wale ndugu zake habari hizo. Mmoja kati yao, yule ndugu wa binamu yake aliyekuwaq akiitwa Hamadi ambaye alikuwa akinichukia sana, alimwambia baba kwamba, ningemsumbua sana huyo mkewe. Baba alisema kwamba, kama ninataka kufa, hapo ndipo palikuwa pahala pazuri pa kufia. Aliongeza kuwambia kwamba, angemtahadharisha sana huyo mke wake mpya kuhusu mimi.

Kweli alioa kwa sherehe ndogo ambayo ilifanyika pale pale nyumbani. Baba alikuwa amepanga nyumba nzima ya vyumba vitatu, tulimokuwa tukiishi. Nilikwambia nilikuwa nikilala sebuleni, unaweza kuhisi kwamba, labda ninajaribu kuongopa. Nitakwambia ni kwa nini baba yangu alikuwa akinichukia.

Baada ya sherehe ile ya ndoa, ambayo ilihusisha ndugu zake yule mama wanne na wale binamu wa baba na mimi ambaye pale nilikuwa kama kijana wa kutumwa, ulifika muda wa mke wa baba kutambulishwa kwa familia. Baba aliwatambulisha wale ndugu zake wawili kwa yule mama mpya. Halafu alimwambia yule mkewe ambaye nilishamchukia hata kabla hajaolewa, ‘huyu ndiye yule mtoto niliyekwambia. Kama akikukera muda wowote naomba nipate taarifaharaka ili nimfunze adabu. Na vitu vyako uviweke vizuri, maana……’

Yule mama yangu mpya wa kamboa aliingilia kati. ‘Sawa nimekuelewa, lakini kwa nini usiniache mwenyewe nikaona kama kweli ni morofi?’ Huyu mama ambye naye alikuwa mtu mzima kidogo, akiwa ni mwalimu aliyewahi kufundisha na baba wakati baba anaanza kazi, alisema huku nikiona wazi kwamba, kauli za baba hazikumshawishi.

Wale ndugu zake baba walicheka na kusema, ‘kwani shemeji tangu uje hujaona kwamba huyu ni mtoto wa mtaani huj….’ Yule mama mpya alimwambia binamu yangu. ‘Nikiwa humu ndani, nisikusikie tena unasema hayo maneno. Nimesema mniache nione mwenyewe, mnanifundisha nini sasa!’ Mama alionekana wazi kwamba alikuwa amekasirika.

Nilihisi kama vile nataka kucheka au kuruka kwa furaha au kulia au sijui kufanyaje, sikujua tu. Hajawahi kuja mgeni pale nyumbani na kuambiwa mambo yangu na kuacha kuwaunga mkono baba na ndugu zake. Yule alikuwa ni mtu wa kwanza. Halafu kumbuka alikuwa ni mama wa kambo ambaye nilitegemea angekuwa katili kuliko baba. Lakini kumbe bado nilikuwa sijagundua jambo kubwa zaidi.

Jioni ile baba na ndugu zake na mkewe ilikuwa watoke kwenda kutembea mjini kukamilisha ile sherehe ya ndoa. Baba alitoka kwenda kwanza dukani na ndugu zake walitoka nao sijui kwenda wapi. Tulibaki mimi na mama yule mgeni.

Kwenye saa 10.30 jioni yule mama alipokuwa ametoka kuswalialiniita na kuingia nami chumbani kwa baba. Nilisita kuingia kwa sababu nilikuwa nimepigwa marufuku hata kusogelea mlango wa chumba hicho, Ingawa binamu zake binamu zake baba walikuwa wakiiba fedha za baba na kudai ni mimi. Ingia Almasi, usiogope mimi ni mama.'

Niliingia na mama aliniambia nikae kitandani. 'Unasikia mwanangu, usikubali kuwa wewe ni mtundu.' Yule mama alianza kusema akiwa amnishika mkono. 'Wewe ni mtoto mzuri, mwenye akili na huruma. Nimekuona ile asubuhi nilipokuja, kwamba, huna tatizo hata kidogo.'

Alinyamaza na kuendelea kusema, 'najua unafahamu kwamba, mama yako alikwishafariki, lakini akina mama wanpofariki, hurudi kwa njia nyingine, kuja kuwapenda tena watoto wao. Nimerudi kuja kukupenda ili usome na kufika mbali sana. Lakini usimwambie mtu. Mimi ni mama yako, nataka nikuone ukiwa shujaa kama wakati ule ulipokuwa mdogo….’ Alitulia kidogo, alikuwa akilia.

Unajua ulipokuwa mdogo ulitambaa na kutembea haraka sana kuliko watoto wengine pale mtaani, hadi watu wakashangaa. Nataka uendelee kuwa mtoto mzuri na mwenye bidii kama wakati ule. Kumbuka kwamba, mimi ni mama nimekuja kukulea.’

Akiwa anafuta machozi aliniambia. ‘Tafuta zile nguo zako nzuri, nikiandalie, jioni tutaenda wote na baba na baba kutembea mjini.’ Nilihisi kitu ambacho hadi leo wala sikijui kilikuwa ni nini. Nilijiona kama siko duniani au sijijui. Nilibubujikwa na machozi na nilisema kwa kunong’ona, ‘sina nguo nzuri.’

Yule mama alisimama na kusema, usijali mwanangu.’ Alikwenda kwenye sanduku lake na alilokuwa amekuja naloasubuhi ile na kulifungua. Alitoa suruali, shati na viatu, vyote vipya. Aliniambia nikaoge, halafu nivae nguo zile.

Nikiwa na kichwa chepesi hadi kufikia kuyumba, bila kujua sababu, nilikwenda kuoga. Nilimwacha mama huku nyuma akiwa bado anafuta machozi yake. Nilirudi bafuni na kuvaa nguo zile. IliIlikuwani mara ya kwanza kwangu kuvaa nguo mpya nikiwa na akili ya kukumbuka, ukiacha sare za shule. Mama alinisifia sana na nilihisi ile hali ambayo sikuwa ninaijua. Hali ngeni kabisa.

Saa 11.30, baba na wale ndugu zake walirudi na awali hakuna aliyenitambua. Waliponitambua, binamu binamu yake baba alisema, ‘umeiba wapi nguo hizo?’Nilimtazama mama ambaye nilikuwa naye pale sebuleni, naye kama kuonyesha kunilinda kam alivyoahidi alisema. ‘Ni mimi nimeiba, Unasemaje?’ Palizuka kimya. Halafu mama alisema maneno ambayo siwezi kuyasahau.

‘Huyu ni mwanangu. Hana tabia mbaya na wala sio mjinga kama mnavyotaka aamini. Huyu ni mtoto mjanja na mwenye uwezo mkubwa wa ufahamu. Nataka niseme hivi. Huyu ndiye atakayeniweka au kuniondoa katika nyumba hii. Akionewa tu, nafunga kilicho changu, naondoka na sioni aibu kusema kwamba nitaondoka naye. Nimemaliza.’ Hakuna aliyejibu labda kwa sababu hakuna aliyeamini.

Alinyamaza na kuendelea kusema, 'najua unafahamu kwamba, mama yako alikwishafariki, lakini akina mama wanapofariki, hurudi kwa njia nyingine, kuja kuwapenda tena watoto wao. Nimerudi kuja kukupenda ili usome na kufika mbali sana. Lakini usimwambie mtu. Mimi ni mama yako, nataka nikuone ukiwa shujaa kama wakati ule ulipokuwa mdogo….’ Alitulia kidogo, alikuwa akilia.

‘Unajua ulipokuwa mdogo ulitambaa na kutembea haraka sana kuliko watoto wengine pale mtaani, hadi watu wakashangaa. Nataka uendelee kuwa mtoto mzuri na mwenye bidii kama wakati ule. Kumbuka kwamba, mimi ni mama nimekuja kukulea.’

Ni kweli hakuna aliyesema neno na sikusikia neno kwa siku ile wala zilizofuata. Wiki ile ile nilianza masomo na wale ndugu zake baba waliondoka miezi miwili tu baadae baada ya kushindwa kuishi na mama ambaye alikuwa ni mtu mnyoofu, anayesema kile ambacho kipo na kinachopaswa kusemwa. Hata baba aliwachukia sana.

Huyu mama ndiye ambaye alimbadili kabisa baba na kumfanya kuwa mtu tofauti kwangu. Nikiwa na umri wa miaka 13 ndipo nilipoanza kujua upendo wa baba na mama.

KWA NINI BABA ALIKUWA ANANICHUKIA? Niligundua kwamba baba katika kuhangaika kwake kwa waganga, aliambiwa kwamba mimi nilizaliwa na mkosi, hivyo kifo cha mama kilikuwa kimepitishwa mikononi mwangu na wachawi na kwamba kama ningekuwa mtu mzima nikiwa kwake, ningesababisha mikosi kwa familia yake. Kwa hiyo baba hakutaka niwe mtu mzima nikiwa kwake.

Mama yangu wa kambo ambaye ndiye mama yangu mzazi kwa ninavyoamini kutokana na upendo wake, ndiye aliyebadili mawazo ya baba ya kishirikina na kumfanya kuanza kufikiri vizuri zaidi kuhusu mimi na maisha kwa ujumla.

Leo hii baba yangu amefariki, lakini mama yangu ninaye, nikiwa na mdogo wangu wa kike ambaye ameolewa na ana shughuli zake, anaitwa Shamim. Huyu mdogo wangu hakuzaliwa na baba yangu, kwani huyu mama mwema alipokuja kuolewa na baba tayari alishaolewa na kuachana na mumewe na walikuwa na mtoto huyo.

Huyu mama ndiye ambaye ameniwezesha kuishi maisha haya ya uadilifu na amani niliyo nayo leo. Ndiye ambaye aliniwezesha kusoma hadi chuo kikuu na kupata ajira na baadae kuanza maisha ya kujitegemea. Ni kweli alikuwa ni mama yangu aliyekuja kunilinda.

Najaribu kufikiria,kuna akina mama wangapi wanoweza kumkubali mtoto wa mwanamke mwingine kama alivyo? Ni wachache kupindukia. Wengi juhudi yao siku zote ni kuona watoto wa kambo wanakorofishana na baba zao, wanateswa na kutupwa nje ya familia. Lakini ni kwa faida ya nani? Siku zote ni kwa hasara zao. Huja kugundua wamepata hasara wakiwa wamechelewa uzeeni.

Ninampenda na nitampenda kuliko mtu mwingine yeyote, mama Zakia Mudani, ambaye amenionesha maana ya kweli kuhusu maisha. Amenifundisha kwamba, suala siyo mama wa kambo, bali ubinadamu, kujua kupenda.

Alikuwa ni mama………………

**************MWISHO***************

1 comment:
Andika Maoni Maoni
  1. Ninanukuu "Alinyamaza na kuendelea kusema, 'najua unafahamu kwamba, mama yako alikwishafariki, lakini akina mama wanpofariki, hurudi kwa njia nyingine, kuja kuwapenda tena watoto wao. Nimerudi kuja kukupenda ili usome na kufika mbali sana. Lakini usimwambie mtu. Mimi ni mama yako, nataka nikuone ukiwa shujaa kama wakati ule ulipokuwa mdogo….’ Alitulia kidogo, alikuwa akilia." mwisho wa kunukuu. Kipande hiki nimerudia kusoma sijui mara ngapi huku machozi yakinititririka. Nimejifunza kitu katika mkasa huu. usengwili!!

    ReplyDelete

This Blog Designed by DonSoo, Contact 0656212326.DonSoo
Kaa Karibu na Mimi