Kila jambo tunafikiri, kutenda, au kusema, kwa sababu ni nguvu, ni lazima lizae matokeo kama hayo au makubwa ama mabaya zaidi. Kama ni baya, litazaa baya zaidi na kama ni zuri litazaa zuri zaidi, huwezi kupanda mahindi, ikaota bangi.
Kama mawazoni mwako kumejaa chuki , vitendo vyako ni vya kiharamia na kauli zako ni za kuchonganisha, basi usitarajie nafuu, kwani kamwe hutaweza kuvuna nafuu kutoka katika mbegu hizo unazopanda. Utavuna ulichopanda, hiyo ni kanuni ya maumbile, huwezi kuibadili.
Kila mtu maisha anayoishi ndiyo uchaguzi wake, ameyapanda mwenyewe na sasa anavuna.
Kama tunataka kupata tunacholenga kwenye maisha yetu, hatuna budi kujua pia tunachopanda kila siku kupitia mawazo, vitendo na kauli zetu.
Kufikiri, mitazamo, imani, hisia,vitendo na kauli, ni mbegu ambazo zinapokuja kuzaa baada ya kupandwa hutuletea mazao tuliyoyapanda. Inawezekana tulisahau au kutojua kwamba, tunapanda mbegu fulani. Hili la kutojua halizuii mbegu hiyo kuzaliwa na kukua, hadi kuvunwa, ikiwa ni ya mmea huo huo.
Jambo la msingi hapa ni kuchagua kupanda kile ambacho mtu anakipenda.
Ruhusu kwenye mawazo yako, imani zako, hisia zako, mitazamo yako, vitendo na kauli zako, yale tu ambayo yatakupa furaha, amani na utulivu.
Pia ambavyo vitakupa ridhiko, upendo na uelewa.